Habari

Siri ya hija takatifu ya Kanisa la Legio Maria

Na GEORGE ODIWUOR July 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KWA Wakenya wengi, Julai Mosi huashiria mwanzo wa mwaka mpya wa kifedha wa serikali lakini kwa waumini wa Kanisa la Legio Maria of African Church Mission, tarehe hiyo ni mojawapo ya siku takatifu zaidi katika kalenda yao ya kidini.

Kila Julai Mosi tangu mwaka 1963, maelfu ya waumini hukusanyika katika Kaunti ya Homa Bay kuadhimisha kuachiliwa huru kwa mwanzilishi wa kanisa hilo, Baba Simeo Melkio Messias Ondeto, aliyekuwa amefungwa katika Gereza la Serikali la Homa Bay.

Kulingana na Papa Lawrence Tilen Kalul, Baba Simeo alikamatwa mwezi Juni na kushtakiwa kwa madai mbalimbali, ikiwemo kuwazuia watu kutafuta matibabu hospitalini na kuwahifadhi wanawake waliotoroka ndoa zao.

Anasema viongozi wa serikali wakati huo walihofia ushawishi mkubwa ambao Baba Simeo alikuwa alipata baada ya kuanzisha kanisa katika eneo la Got Kweru (Got Calvary), Kadem, ambako maelfu ya watu walikuwa wakimiminika kutafuta maombi na ushauri wa kiroho.

“Serikali ilitaka kujua alikuwa akifanya nini huko Got Kweru kwa sababu watu walikuwa wanazidi kumiminika,” alisema Papa Lawrence.

Kwa mujibu wa viongozi wa kanisa hilo, Baba Simeo aliachiliwa baada ya siku 30 gerezani kufuatia matukio yaliyodaiwa kuwa ya kimiujiza yaliyotokea akiwa kifungoni.

Papa Lawrence anadai kuwa Baba Simeo hakula chakula akiwa gerezani lakini hakudhoofika wala kuugua.

“Usiku macho yake yalikuwa yaking’aa na kuangaza seli nzima baada ya taa kuzimwa,” alidai.

Waumini pia husimulia kuwa mkuu mmoja wa gereza aliwahi kumwona Baba Simeo akiwa nje ya seli kabla hata milango ya gereza kufunguliwa, huku walinzi wengine wakidai hawakumuona.

Hadithi nyingine inayosimuliwa mara kwa mara ni ya Jaji Ogot, aliyemhukumu Baba Simeo. Inadaiwa kuwa baada ya kumuona gerezani, baadaye alimuona tena akiwa nje ya gereza, jambo lililomshangaza na kumfanya kurejea gerezani kuthibitisha kama bado alikuwa ndani.

Waumini huamini matukio hayo ndiyo yaliyochangia kuachiliwa kwake.

Maadhimisho huanza alfajiri ambapo maelfu ya waumini kutoka sehemu mbalimbali za nchi husafiri hadi Homa Bay na kukutana Junction Kodoyo kabla ya kuanza hija rasmi.

Kutoka hapo hutembea hadi soko la samaki katika mwambao wa Ziwa Victoria ambako hufanya maombi ya kuliombea taifa, kisha kuelekea Gereza la Homa Bay.

Waumini hao huvaa kanzu za rangi mbalimbali zikiwemo nyekundu, bluu, kijani, nyeupe, kahawia na machungwa. Wengi hutembea wakiwa wamevaa viatu vya maarufu kama akala vilivyotengenezwa kwa tairi za magari huku wengine wakitembea bila viatu.

Shingoni mwao hutundika rozari na picha za Baba Simeo, huku wakisalimiana kwa maneno ‘Wuod Baba’, yanayomaanisha mwana wa Baba.

Mbele ya msafara huo huongozwa na kundi linalojulikana kama Jeshi la Malaika Mkuu Mikaeli, wanaume na wanawake wanaovalia mavazi mekundu.
Hawa hubeba bunduki, mapanga, visu na kombeo za mbao zinazoonekana kama silaha halisi.

Papa Lawrence anasema silaha hizo ni ishara ya vita vya kiroho dhidi ya nguvu za uovu, zikichochewa na simulizi za Biblia kuhusu Malaika Mkuu Mikaeli, anayejulikana kama mlinzi wa waumini na kamanda wa majeshi ya mbinguni.

Baadhi ya waumini pia hubeba funguo kubwa za mbao kuashiria mafundisho ya Injili ya Mathayo 16:19 kuhusu “funguo za ufalme wa mbinguni.”

Msafara unapofika gerezani, shughuli za kawaida husimamishwa kwa muda huku maafisa wa magereza wakihakikisha usalama wa maelfu ya mahujaji wanaoingia kufanya ibada.

Baada ya mapumziko mafupi, Misa huanza. Waumini huimba nyimbo za sifa, kupiga magoti na wengine huzungumza kwa lugha wanazoamini ni za kiroho.

Wazee wa kanisa huhakikisha taratibu zote za ibada zinafuatwa, huku wanaovaa viatu wakitakiwa kuvivua na wanaotembea wakati wa maombi kuamriwa kupiga magoti.

Baada ya ibada katika gereza hilo, mahujaji huendelea na safari ya zaidi ya kilomita 10 hadi St Margaret Chiga, ambako viongozi wakuu wa kanisa, akiwemo Papa Lawrence na Kardinali Camerlengo Joseph M. Ong’awo Aloo, huongoza ibada nyingine.

Padri Bernadus Ochieng Rafael wa St Joseph Judea Ongo, Rongo, anasema ameshiriki hija hiyo tangu alipokuwa mtoto.

“Hija hii huimarisha imani yetu na hutukutanisha waumini kutoka maeneo mbalimbali ya Kenya. Pia matembezi haya huchangia afya njema kwa kusaidia kudhibiti kiwango cha sukari mwilini,” alisema.

Kwa waumini wa Legio Maria, hija ya Julai Mosi si desturi tu bali ni sehemu muhimu ya maisha yao ya kiroho, na wengi hujitahidi kuhudhuria kila mwaka hata kama hawana fedha za kurejea nyumbani, wakiamini Mungu atawafungulia njia.