Siri ya ziara ya Gachagua Amerika
KIONGOZI wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, anatarajiwa kuanza rasmi shughuli zake za kisiasa nchini Amerika kesho Jumatatu baada ya kukamilisha mapumziko ya siku 10 akiwa pamoja na mkewe, Mchungaji Dorcas Rigathi.
Bw Gachagua, ambaye aliondoka nchini Agosti 26 kuelekea Amerika, alisema aliamua kwanza kutumia muda wa faragha na familia kabla ya kuanza mikutano yake ya kisiasa na wafuasi wa chama hicho walio Amerika.
Mwanasiasa huyo amekuwa akichapisha picha akiwa na mkewe wakifurahia mapumziko, ikiwemo safari za boti zenye mwendo kasi na matembezi asubuhi.
“Familia ni muhimu sana. Nilihitaji kwanza kupata muda wa kutosha pamoja na mke wangu ambaye ameendelea kunipa nafasi ya kushughulikia siasa nyumbani Kenya. Baada ya mapumziko hayo nitaanza mikutano ya kisiasa kuhusu hali ya nchi, umuhimu wa kujenga DCP, haja ya kuwa na mgombea mmoja wa urais wa upinzani, pamoja na malengo na bajeti yetu,” alisema Gachagua.
Kiongozi huyo wa DCP alisema atakuwa na mikutano ya hadhara na ya faragha huku akijaribu kujenga chama chake kama mshirika muhimu katika juhudi za kuleta mabadiliko ya kisiasa nchini Kenya kupitia njia za kidemokrasia.
Alisema mojawapo ya malengo yake ni kuhimiza muungano wa upinzani kutafuta viongozi bora watakaowania nyadhifa mbalimbali katika serikali ya kitaifa na za kaunti.
“Nitakutana na wafuasi kutoka Mlima Kenya na sehemu nyingine za nchi. Tumeanzisha sera ya kukusanya wote na kutomtenga yeyote ndani ya DCP. Tunauza maono ya chama na ajenda ya kitaifa kuhusu kwa nini ni muhimu kuondoa Kenya katika hali ya sasa chini ya utawala wa Rais William Ruto. Tuna malengo, mikakati na pia pengo la kifedha ambalo tunahitaji kuziba,” alisema.
Kwa mujibu wa Gachagua, siku 45 zijazo atakazokuwa Amerika zitalenga kutafuta uungwaji mkono kisiasa na kifedha kutoka kwa Wakenya wanaoishi ughaibuni kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Ratiba iliyotolewa na DCP inaonyesha kwamba hadi Septemba 10 atakuwa katika mji wa Spokane, jimbo la Washington, ambako atahudhuria mikutano ya hadhara pamoja na vikao vya faragha na watu wanaotajwa kuwa muhimu kwa ajenda ya chama.