Habari

Visa vya utapeli mitandaoni vyaongezeka nchini

Na ERIC MATARA April 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAKENYA wanaendelea kunaswa na matapeli kutokana na ukosefu wa ajira, tamaa ya kupata pesa kwa haraka na mbinu za kisasa zinazotumiwa na wahalifu mtandaoni.
Visa vya hivi karibuni vinaonyesha jinsi ulaghai unavyozidi kuwa wa hali ya juu na wenye kushawishi.
Kwa mfano, Bi Lillian Chemitei, mwenye umri wa miaka 35, aliangukia tangazo la kazi aliloliona kwenye Facebook kutoka kampuni inayodaiwa kuwa Nairobi.
Baada ya kuwasilisha ombi lake, aliitwa kwa mahojiano katika hoteli moja jijini Nairobi.
Hata hivyo, yeye na waombaji wengine waliporwa simu, vipakatalishi na mali yote waliyokuwa nayo , pamoja na ada ya Sh5,000 waliyodaiwa kulipa kama “gharama ya mahojiano”.
Kisa hiki si cha kipekee. Katika tukio jingine, maafisa wa Idara ya Uchunguzi wa Jinai (DCI) walimkamata mshukiwa mmoja aliyekuwa akiwahadaa watu kwa ahadi ya kuwapa ajira ya polisi baada ya kulipwa mamia ya maelfu ya pesa.
Wengine walinaswa wakiuza barua bandia za kujiunga na Huduma ya Polisi.
Kwa wengi, tamaa ya kupata ajira au kipato cha haraka huwafanya kupuuza tahadhari muhimu.
John (sio jina lake halisi), mhitimu wa uhandisi kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi, alitapeliwa Sh20,000 baada ya kuahidiwa kazi kupitia tangazo la mtandaoni.
Baada ya kutuma fedha, aliyekuwa akiwasiliana naye alitoweka.
Katika Kaunti ya Kiambu, DCI ilivunja mtandao uliokuwa ukitumia ukurasa bandia unaojifanya kuwa Jumia Kenya kuwahadaa wateja kwa bei za kuvutia.
Mteja mmoja alipoteza Sh105,000 baada ya kulipa bidhaa ambazo hazikuwahi kuwasilishwa.
Wataalamu wanasema sababu kuu ya hali hii ni ukosefu wa ajira, hasa miongoni mwa vijana, unaowasukuma wengi kufanya maamuzi ya haraka bila uchunguzi wa kina.
Dkt James Ombati anasema hali ya kukata tamaa huwafanya watu kuwa rahisi kudanganywa.
Aidha, shinikizo la kijamii la kutaka utajiri wa haraka linaongeza hatari hiyo.
Wakili Steve Kabita anaeleza kuwa mapengo ya kisheria yanachangia kuenea kwa utapeli.
Anasema wahalifu wengi hujikuta wakihepa mkono wa sheria au kusuluhisha kesi nje ya mahakama, kisha kurejea kwa mbinu mpya za ulaghai.
Kwa miaka miwili iliyopita, Wakenya wamepoteza takriban Sh10 bilioni kupitia miradi ya uwekezaji hewa.
Utafiti mmoja umeonyesha kuwa asilimia 82 ya waliowekeza katika mipango ya “faida kubwa” walipoteza fedha zao.
Mashirika ya umma na binafsi pia yamekuwa yakitoa tahadhari mara kwa mara.
Kampuni kama Kenya Railways, Geothermal Development Company na Tana Water Works Development Agency zimeonya dhidi ya matangazo bandia ya kazi na zabuni.
Mkurugenzi wa DCI, Mohamed Amin, anashauri wananchi kuwa makini zaidi.
Anasisitiza kuwa tangazo lolote linaloonekana kuwa nzuri kupita kiasi mara nyingi huwa na dosari.
Pia anahimiza wananchi kuthibitisha taarifa kabla ya kutuma fedha au kufichua data nyeti kama neno siri.
Teknolojia inavyoendelea, matapeli nao wanazidi kubuni mbinu mpya, ikiwa ni pamoja na kutumia Akili Unde (AI) kuunda matangazo yanayoonekana halisi.
Hali hii inaweka wazi kuwa mapambano dhidi ya utapeli yanahitaji uangalifu wa hali ya juu kutoka kwa wananchi pamoja na hatua kali za kisheria dhidi ya wahalifu.