Wapwani wavuna kwenye bajeti ya Ruto
ENEO la Pwani limeibuka kuwa miongoni mwa yaliyofaidika kwa kupata mgao mkubwa zaidi katika Bajeti ya Taifa ya mwaka wa fedha 2026/27, huku serikali ikitenga Sh5 bilioni za kununua ardhi kwa ajili ya maskwota.
Akiwasilisha makadirio ya bajeti mbele ya Bunge la Taifa mnamo Alhamisi iliyopita, Waziri wa Fedha, Bw John Mbadi, alisema fedha hizo ni sehemu ya mpango mpana wa Sh9.4 bilioni wa kuwapa makazi rasmi watu wasio na ardhi kote nchini.
Hatua hiyo imetokea karibu mwezi mmoja baada ya Rais William Ruto kuzuru eneo la Pwani na kuahidi kutenga fedha za kununua ardhi kutoka kwa wamiliki wasiokuwepo na kuwapa maskwota.
Waziri wa Madini, Uchumi wa Bahari na Masuala ya Ubaharia, Bw Hassan Joho, alisema mgao huo unaonyesha dhamira ya serikali ya kutatua tatizo la ardhi ambalo limeisumbua Pwani kwa zaidi ya miongo sita tangu Kenya ipate uhuru.
“Kwa miaka mingi, watu wa Pwani wamekuwa wakilalamikia suala la ardhi. Mgao huu unaonyesha kwamba serikali imeamua kushughulikia tatizo hili kwa njia ya kudumu. Hili ni jambo ambalo wakazi wamekuwa wakilisubiri kwa muda mrefu,” alisema Bw Joho.
Aliongeza kuwa, umiliki wa ardhi unasalia kuwa mojawapo ya vikwazo vikubwa kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika eneo hilo.
Katika mpango huo, serikali imependekeza kutenga Sh892 milioni kwa ajili ya utathmini na usajili wa hati miliki za ardhi na Sh388 milioni kwa uwekaji wa kumbukumbu za ardhi katika mfumo wa kidijitali.
Hatua hizo zinalenga kuimarisha usalama wa umiliki wa ardhi, kupunguza migogoro ya ardhi na kufungua fursa za uwekezaji.
Pwani pia imetengewa fedha za kustawisha sekta za uchukuzi, uvuvi, uchumi wa baharini na miundomsingi ya usafirishaji wa bidhaa.
Wizara ya Fedha ilitangaza kuwa, imetenga Sh400 milioni kwa ajili ya kivuko cha feri Likoni, Mombasa.
Hata hivyo, kiasi hicho ni kidogo ikilinganishwa na ahadi ya awali ya Rais Ruto ya Sh3 bilioni za kununua feri mpya ili kuboresha huduma katika eneo hilo.
Wizara imependekeza pia kutenga Sh8.2 bilioni kwa sekta ndogo ya Uchumi wa Bahari na Uvuvi.
Fedha hizo zinajumuisha Sh2.1 bilioni kwa Mradi wa Maendeleo ya Biashara ya Ufugaji Samaki, Sh1.8 bilioni kwa Mradi wa Maendeleo ya Uvuvi wa Baharini na Kijamii na Kiuchumi wa Kenya, pamoja na Sh578 milioni kwa Kituo cha Mafunzo ya Uvuvi na Ufugaji Samaki cha Kabonyo kilicho Kisumu.
Pwani pia itanufaika na kukamilika kwa uwekezaji unaoendelea katika miundombinu ya maeneo ya kutua samaki, ambapo vituo vya kisasa vinaendelea kujengwa katika kaunti tano. Miradi hiyo imepangwa kukamilika ifikapo mwisho wa mwezi huu.
Serikali ilisema inaendelea kushirikiana na sekta binafsi kuboresha vituo vya makontena, magati ya mizigo, vituo vya ndani vya makontena na maeneo maalum ya kiuchumi katika Kaunti za Mombasa na Lamu, pamoja na miradi mingine Nairobi na Naivasha.
Uwekezaji huo unatarajiwa kuimarisha nafasi ya Kenya kama kitovu kikuu cha biashara na usafirishaji wa bidhaa Afrika Mashariki huku ukifungua fursa mpya za kiuchumi kwa kaunti za Pwani.