Habari

Wakenya 40,000 wamefariki katika ajali za barabarani miaka 10-Ripoti

Na PIUS MAUNDU Na PETER MBURU August 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

AJALI  za barabarani zimeendelea kuwa tishio kubwa Kenya, huku zaidi ya watu 40,000 wakifariki katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, kulingana na takwimu za serikali.
Jana, huzuni ilitanda eneo la Nthongoni, Kaunti ya Makueni, baada ya ajali mbaya ya barabarani kusababisha vifo vya watu saba na kujeruhi zaidi ya 60. Abiria walikuwa wakielekea sherehe ya kulipa mahari katika kijiji cha Inyoni, safari iliyotarajiwa kuwa ya furaha ikageuka kuwa ya majonzi.
Kiongozi wa jamii Joseph Kyonda alieleza kuwa alipoteza majirani sita na kuomba msaada wa kifedha kwa mazishi yenye heshima.
Basi dogo lenye viti 46 lilikuwa limebeba watu 71 wakati ajali ilitokea. Afisa Mkuu wa Afya wa Kaunti, Harvey Mulei, alisema Hospitali ya Matiliku ilipokea majeruhi 28 na Hospitali ya Rufaa ya Makueni ikapokea 36. Manusura walieleza kuwa taa za gari zilikatika kabla ya kuacha barabara na kutumbukia shimoni.
Haya yanajiri huku takwimu zikionyesha kuwa miundombinu duni ya barabara, ukosefu wa madaraja ya watembeao kwa miguu na alama za trafiki na uzembe wa madereva na watembea kwa miguu ni sababu nyingi zinazochangia ongezeko la vifo na majeraha barabarani.
Hata hivyo, Shirika la Afya Duniani (WHO) linaonya kuwa idadi halisi ya vifo inaweza kuwa kubwa zaidi kuliko inavyoonyeshwa na takwimu rasmi. WHO inaeleza kwamba, Kenya huhesabu tu vifo vinavyotokea mara moja baada ya ajali, huku wengi wanaofariki hospitalini siku au miezi kadhaa baadaye wakiachwa nje ya rekodi hizo.
Kwa mujibu wa Shirika la Kitaifa kuhusu Takwimu Kenya (KNBS), watu 114,466 walihusika katika ajali za barabarani kati ya 2021 na 2025. Katika kipindi hicho, watu 22,894 walifariki huku zaidi ya 90,000 wakijeruhiwa.
 Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama Barabarani (NTSA) inasema ongezeko la idadi ya watu, magari na msongamano wa trafiki limefanya hali kuwa mbaya zaidi.