Wasichana 9 wa Utumishi Girls wanaoshukiwa kuchoma bweni watupwa rumande
MAHAKAMA ya Naivasha imeamuru wanafunzi tisa wa Shule ya Wasichana ya Utumishi Senior School wanaoshukiwa kuhusika na uchomaji wa bweni uliosababisha vifo vya wanafunzi 16 wazuiliwe kwa siku 21 huku polisi wakiendelea na uchunguzi.
Mahakama ilitoa uamuzi huo baada ya upande wa mashtaka kuomba muda zaidi wa kuwazuilia wanafunzi hao ili kukamilisha uchunguzi kuhusu mkasa huo uliotokea usiku wa Mei 27 na 28.
Hakimu Mkuu alisema sababu kuu za kuidhinisha ombi hilo ni usalama wa wanafunzi hao pamoja na uwezekano wa kuingilia mashahidi wa kesi hiyo.
Wanafunzi hao watazuiliwa katika Kituo cha Watoto cha Nakuru hadi Juni 24 kesi hiyo itakapotajwa tena.
“Nimeridhika kuwa kuna uwezekano wa kuingiliwa kwa mashahidi, jambo ambalo ni sababu ya msingi. Hata hivyo, sababu kubwa zaidi ni usalama wa washukiwa hawa,” alisema hakimu katika uamuzi wake.
Mahakama ilikubaliana na upande wa mashtaka kuwa tukio hilo limezua hasira kubwa miongoni mwa umma.