Wimbi la vurugu lagubika shule likiacha uharibifu, majeraha na vifo
WIMBI la vurugu limekumba shule kadhaa nchini na kuacha nyuma uharibifu wa mali, kufungwa kwa baadhi ya taasisi, majeruhi na vifo katika visa vya kusikitisha vinavyozidi kuzua hofu miongoni mwa wazazi na wadau wa elimu.
Matukio hayo sasa yameibua mjadala kuhusu usalama wa wanafunzi, nidhamu shuleni na ufanisi wa mifumo ya usimamizi wa elimu, huku shule kadhaa zikilazimika kufungwa kwa muda au kwa muda usiojulikana.
Hali hiyo inajiri baada ya tukio la kutisha la Machi 28, 2026, katika Shule ya Upili ya Wasichana ya Utumishi, Gilgil, Kaunti ya Nakuru, ambapo moto ulioteketeza bweni uliua wanafunzi 16 na kujeruhi wengine 79.
Mkasa huo umeacha biwi la simanzi kitaifa na kuchochea wito wa kuimarishwa kwa viwango vya usalama shuleni, hususan mifumo ya kuzuia na kuzima moto.
Wizara ya Elimu imesema ongezeko la matukio ya vurugu linachangiwa na mchanganyiko wa hofu ya mitihani, msongo wa mawazo kwa wanafunzi, malalamishi kuhusu huduma shuleni kama chakula na maji, pamoja na mawasiliano duni kati ya uongozi wa shule na wanafunzi.
Katibu wa Elimu, Profesa Julius Bitok, amesema serikali imechukua hatua za haraka kudhibiti hali hiyo kwa kuagiza ukaguzi wa kitaifa katika shule zote ndani ya wiki mbili ili kubaini chanzo cha matatizo hayo na kuyatatua kabla hayajazidi.
Aidha, alisema idadi ya maafisa wa ubora wa elimu imeongezwa kutoka 600 hadi 1,000 ili kuimarisha ufuatiliaji wa shule na kusaidia katika kutatua migogoro mapema.
“Baadhi ya matukio haya yanatokana na hofu ya mitihani, lakini pia kuna changamoto za mawasiliano na uongozi wa shule. Tunawahimiza walimu kusikiliza wanafunzi na kushughulikia malalamishi mapema,” alisema Prof Bitok.
Hata hivyo, serikali imeonya pia kuhusu uwezekano wa matukio haya kuchochewa na kile ilichoita “tabia ya kuiga” kutokana na taarifa nyingi za vyombo vya habari, hali inayoweza kuwafanya wengine kuiga matukio ya vurugu au uchomaji wa mali.
Kwa upande wake, mwenyekiti wa Chama cha Wazazi, Silas Obuhatsa, amepinga kauli za serikali kwamba matukio haya ni ya “kawaida au ya pekee”, akisema hali ilivyo ni ya dharura ya kitaifa inayohitaji hatua za haraka.
“Shule zinawashwa moto kote nchini na watoto wetu wako hatarini. Hatuwezi kuita haya matukio ya pekee wakati shule nyingi zinafungwa na mali kuharibiwa,” alisema.
Bw Obuhatsa ameitaka Wizara ya Elimu kuhakikisha sera za usalama shuleni zinatekelezwa kikamilifu, akibainisha kuwa sehemu kubwa ya miongozo ya usalama ipo kwenye karatasi lakini haijatekelezwa kwa vitendo.
Zaidi ya shule 18 za bweni zimeathiriwa na vurugu au matukio ya moto tangu Aprili, hasa katika Nakuru, Murang’a, Embu, Kisii, Siaya, Makueni na maeneo ya Pwani.
Baadhi ya shule zilizofungwa ni pamoja na St Joseph Seminary Molo, Naivasha Girls, Moi Forces Academy Lanet na Saseta Girls Bomet.
Katika baadhi ya matukio, wanafunzi walirudishwa nyumbani kwa muda usiojulikana ili kuruhusu uchunguzi na tathmini ya usalama.
Kaunti ya Nakuru imeathirika pakubwa. Shule zilizofungwa au kuathirika ni pamoja na St Joseph Seminary Molo, Naivasha Girls, Moi Forces Academy Lanet, Utumishi Girls Academy Gilgil, pamoja na Kabarak na Shule ya Wavulana ya Subukia.
Katika Murang’a, shule kadhaa zimekumbwa na moto na vurugu, zikiwemo za sekondari za Weithaga, ya wavulana ya Kiaguthu, ya wavulana ya Kirogo, ya wasichana ya Kahuhia, ya wasichana ya Nginda, pamoja na ya wavulana ya Kiria-ini.
Kaunti ya Embu ni moja ya kaunti zilizoathirika zaidi, ambapo zaidi ya shule 15 zimekumbwa na migogoro.
Miongoni mwao ni za wavulana na wavulana za Kangaru, ya wasichana ya Sacred Heart Kyeni, ya wavulana ya Kianjokoma na ya wasichana ya Githimu na ya mseto ya Kimangaru.
Katika Kisii, visa vya moto na vurugu vimeripotiwa katika shule za wavulana ya Sameta, Nyakeiri, Magena, St John’s Nyamagwa, pamoja na shule ya msingi ya St Mary’s Nyamagwa ambapo uharibifu wa mali ulitokea.
Katika Siaya, shule ya bweni ya wavulana ya Barding ilifungwa baada ya kugunduliwa mpango wa mgomo. Pia za wavulana za Sirembe na Sawagongo ziliripotiwa kuwa katika hali tete.
Makueni pia imeathirika, ambapo shule zilizofungwa ni pamoja na ya wavulana ya Kaumoni, Kalama, Kavuthu, Kyamuthei, na Nguumo, zote zikihusishwa na vurugu au uchomaji wa mabweni.
Katika ukanda wa Pwani, zaidi ya shule 18 zimeathirika tangu Aprili. Miongoni mwao ni shule ya sekondari ya Dr Aggrey, ya wasichana ya Mwasere, Kenyatta (Taita Taveta), ya wavulana ya Voi, ya wasichana ya Bura, na Rabai (Kilifi).
Wataalamu wa elimu wanasema mchanganyiko wa msongo wa mitihani, mawasiliano duni na ukosefu wa huduma bora za kimsingi umechangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa vurugu hizo.
Wito sasa umetolewa wa kuimarisha ushauri nasaha mashuleni, kuboresha mawasiliano kati ya walimu, wazazi na wanafunzi, na kuongeza uwekezaji katika miundombinu ya usalama.
Wadau wanasema bila hatua za haraka, wimbi hili linaweza kuendelea kuathiri mfumo wa elimu na kuleta athari za muda mrefu kwa ustawi wa wanafunzi na maendeleo ya taifa kwa ujumla.