Watoto laki moja hawajapata chanjo za magonjwa hatari
ZAIDI ya watoto wachanga 100,000 waliozaliwa kati ya Januari na Juni 2025 bado hawajapokea chanjo muhimu dhidi ya magonjwa hatari ya utotoni, kwa mujibu wa data kutoka Kenya Health Information System (KHIS).
Takwimu hizo zinaashiria tatizo kubwa linaotishia kufuta mafanikio ya miongo kadhaa katika kulinda afya ya watoto nchini.
Idadi hiyo huenda ikawa kubwa zaidi kwani data hiyo inahusisha tu watoto waliozaliwa katika vituo vya afya.
Watoto waliozaliwa nyumbani hawakuhesabiwa, na hivyo wako katika hatari ya kuambukizwa magonjwa kama ukambi, polio, kifua kikuu, na mengineyo yanayoweza kusababisha ulemavu maishani au hata kifo.
Katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Kakamega, Bi Priscilla Shitoka, mama wa watoto watatu mwenye umri wa miaka 30, aketi kwenye benchi akibeba mwanawe wa miezi sita aliyezaliwa Januari 4, ambaye bado hajapokea hata dozi moja ya chanjo.
Akiwa amechoshwa na safari za kutafuta chanjo, Shitoka anasema:“Nimetembelea vituo 15 vya afya kutoka kiwango cha kwanza hadi cha nne katika kaunti hii bila mafanikio. Mwanangu hajapata hata sindano moja ya chanjo tangu azaliwe. Usiku silali, naishi kwa hofu.”
Anasema katika kijiji cha Shikhambi anakoishi, akina mama wengine zaidi ya 50 pia wako katika hali kama yake, wakiwa na watoto ambao hawajachanjwa hata mara moja.
Swali linalowakumba wazazi kama Shitoka ni ikiwa kuna maana yoyote kuchanja watoto wao miezi sita baada ya kukosa ratiba ya kawaida ya chanjo. “Chanjo ya miezi sita baada ya kuzaliwa bado itasaidia? Afya ya mtoto wangu itadhurika?” anauliza kwa wasiwasi.
Katika Kaunti ya Garissa, hali ni ya wasiwasi pia. Hamza Aden, 26 aliyejifungua mtoto wa kwanza asema:“Mtoto wangu alipata tu chanjo ya Polio wakati wa kampeni ya dharura mwezi Aprili. Rafiki yangu alimpoteza mtoto kwa sababu ya ukosefu wa chanjo, sina amani hata kidogo.”
Kwa mujibu wa Wizara ya Afya, visa 14 vya polio vilithibitishwa Garissa mwezi Januari, hali iliyosababisha kampeni ya haraka ya kuchanja zaidi ya watoto 300,000.
Hata hivyo, kwa watoto waliozaliwa baada ya kampeni hiyo, changamoto bado ipo.Katika hatua ya kutuliza hofu ya wazazi, Waziri wa Afya 3 alitangaza kuwasili kwa dozi 3 milioni za chanjo ya kifua kikuu (BCG) na dozi milioni 3.2 za chanjo ya polio.
“Serikali imehakikisha kuwa fedha za chanjo haziwezi kupunguzwa wala kucheleweshwa. Tunatoa wito kwa wazazi wote kuwapeleka watoto wao kupokea chanjo hizo mara moja,” alisema Duale.
Hata hivyo, alionya kuhusu upungufu wa kimataifa wa chanjo ya rotavirus unaotarajiwa katika robo ya mwisho ya 2025, akisema juhudi zinaendelea kuhakikisha Kenya hainyimwi chanjo hiyo.
Katibu wa Huduma za Matibabu, Dkt Ouma Oluga, alidokeza kuwa serikali inajiandaa kuanzisha kampeni maalum ili kuhakikisha watoto wote waliokosa chanjo katika miezi sita iliyopita wanapata kabla ya Julai kuisha: “Hakuna hospitali, mhudumu wa afya wala mzazi anayepaswa kuwa na hofu. Tutafikia watoto wote.”
Huku serikali ikichukua hatua kurekebisha hali, maelfu ya wazazi nchini bado wanahangaika, wakiwa na hofu kuhusu mustakabali wa kiafya wa watoto wao kutokana na ucheleweshaji huu wa chanjo.