Brazil kumenyana na Japan, Ujerumani ikivaana na Paraguay raundi ya 32 Kombe la Dunia
MABINGWA mara tano wa Kombe la Dunia Brazil watashuka dimbani Jumatatu usiku kumenyana na Japan katika mechi ya raundi ya 32 wakisaka tiketi ya kutinga raundi ya 16 bora.
Brazil walimaliza kileleni mwa Kundi C baada ya kuanza kwa sare ya 1-1 dhidi ya Morocco kabla ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Haiti na Scotland. Vinicius Junior na Matheus Cunha wamekuwa nguzo muhimu katika safu ya ushambuliaji ya kikosi cha kocha Carlo Ancelotti.
Brazil imefuzu hatua hii katika kila Kombe la Dunia tangu 1982 na itaingia mechi hii ikiwa imeandika ushindi mara tano katika mechi sita zilizopita, huku pia ikidumisha mechi mbili mfululizo bila kuruhusu bao.
Hata hivyo, Japan imeonyesha kuwa si wapinzani wa kudharariliwa. Samurai Blue waliwashangaza Brazil kwa ushindi wa 3-2 katika mechi ya kirafiki Oktoba mwaka jana, ushindi wao wa kwanza dhidi ya Selecao.
Japan walifuzu kama washindi wa pili wa Kundi F baada ya sare ya 1-1 dhidi ya Uswidi. Mlinda lango Zion Suzuki aliokoa mashuti kadhaa na kuisaidia timu yake kusalia nafasi ya pili.
Wakati huo huo, Ujerumani waliongoza Kundi E baada ya kuwafunga Curacao na Ivory Coast kabla ya kupoteza mechi yao ya mwisho 2-1 dhidi ya Ecuador.
Kikosi cha Julian Nagelsmann hakikuwa miongoni mwa timu zilizotajwa kuwa wagombea wakuu wa ubingwa, lakini bado kinaamini kina uwezo wa kusonga mbele.
Paraguay walifuzu kama mojawapo ya timu bora zilizomaliza nafasi ya tatu, wakikusanya pointi nne katika Kundi D na kukosa nafasi ya pili kwa tofauti ya mabao dhidi ya Australia.
Timu hiyo ya Gustavo Alfaro iliifunga Uturuki 1-0 na kutoka sare tasa dhidi ya Australia ili kujihakikishia tiketi ya hatua hii.
Ujerumani watamkosa beki Nico Schlotterbeck kutokana na jeraha la kifundo cha mguu, huku Antonio Rudiger na Jonathan Tah wakitarajiwa kuongoza safu ya ulinzi. Kai Havertz, Florian Wirtz na Jamal Musiala wataendelea kuongoza mashambulizi.
Kwa upande wa Paraguay, Diego Gomez hatacheza mechi hii kutokana na kadi za njano, lakini Miguel Almiron anarejea baada ya kutumikia adhabu yake.
Ingawa Paraguay wana uwezo wa kuisumbua Ujerumani, uzoefu na ubora wa Wajerumani unawapa nafasi kubwa ya kufuzu raundi ya 16 bora.