Wito viongozi wawajibike
MWANAHARAKATI Francis Awino, ametoa wito kwa ukaguzi wa umma, ushirikishwaji wa wananchi na uwajibikaji katika uongozi wa vyama vya wafanyakazi.
Akizungumza katika hotuba ya hadhara Alhamisi Aprili 2, 2026, Awino alisema kuna haja ya kuimarisha ushirikiano kati ya wanaharakati, na taasisi za kielimu ili kujenga jamii yenye uelewa mpana wa masuala ya utawala.
“Wananchi wanahitaji viongozi ambao watawajibika na kuwatumikia ipasavyo,” akasema Bw Awino.
Alipendekeza kuanzishwa kwa majukwaa maalum yatakayowawezesha wanafunzi kushirikiana moja kwa moja na wanaharakati na wataalamu wa masuala ya kijamii ili kukuza taifa linalofikiri kwa kina.
Awino pia aliwakashifu viongozi wanaong’ang’ania madarakani bila uwazi, akisisitiza kuwa matokeo yoyote yenye utata yanapaswa kufutwa na kufanyiwa ukaguzi huru.
Awino alisema wanaharakati wanataka rekodi za fedha zilizokaguliwa ili kuhakikisha michango ya wafanyakazi inasimamiwa kwa uwazi.
Kwa mujibu wa historia, Kenya imekumbwa na changamoto za uwajibikaji katika vyama vya wafanyakazi, huku malalamishi kuhusu matumizi mabaya ya fedha na uongozi wa muda mrefu yakijitokeza mara kwa mara.
Haya yanajiri siku chache baada ya vuguvugu la Mtetezi kuwasilisha kesi mahakamani kupinga kuchaguliwa tena kwa Francis Atwoli kama Katibu Mkuu wa COTU-K.
Katika ombi hilo, mwanaharakati huyo alitaka kusimamishwa kwa utekelezaji wa matokeo ya uchaguzi huo, ikiwa ni pamoja na kutambuliwa kwa Francis Atwoli kama Katibu Mkuu wa COTU.
“Kukosa kutoa taarifa muhimu ni ukiukaji wa Katiba na kunanyima wafanyakazi haki ya kushiriki kikamilifu katika uongozi wa vyama vyao,” sehemu ya taarifa hiyo ilisoma.