JIFUNZE LUGHA: Ni neno gani mwafaka kati ya ‘onesha’ au ‘onyesha’?
MWAKA wa 2014, katika mojawapo ya warsha za uhariri wa kamusi, uliibuka mjadala kuhusu maneno ‘onesha’ na ‘onyesha’.
Baadhi ya wataalamu walidai kuwa neno mwafaka linalopaswa kutumiwa wakati wa kueleza kitendo cha kumfanya mtu kuona ni ‘onesha’ bali si ‘onyesha’.
Kundi hili lilikuwa na sababu tatu zilizolifanya kushikilia kuwa ‘onyesha’ ni neno ambalo kwa muda mrefu limekuwa likitumiwa kimakosa hivyo basi watu wanapaswa kujifunza upya.
Sababu ya kwanza inahusu mabadiliko ya sauti ambayo hutokea katika kauli ya kutendesha. Katika jumla ya mabadiliko hayo ambayo ni pamoja na |iz|, |ez|, |ish|, |esh|, |liz|, |lez|, |lish|, |fy|, |vy| na |lesh|, hapana popote ambapo sauti |ny| hujitokeza. Kwa hivyo, kwa kuzingatia sheria zote zinazoongoza mifanyiko ya sauti, kauli ya kutendesha ya kitenzi hicho ni ‘onesha’ wala si ‘onyesha’.
Sababu ya pili ilijikita katika kauli nyingine za kitenzi ‘ona’. Kwa mfano, tunasema ‘onea’ wala si ‘onyea’, ‘onelea’ wala si ‘onyelea’, ‘onewa’ wala si ‘onyewa’, ‘onwa’ wala si ‘onywa’ miongoni mwa mabadiliko mengine ya sauti. Hatimaye, lilidai kuwa kitenzi ‘ona’ kinaponominishwa, tunapata nomino ‘oni’ au ‘maoni’ wala si ‘onyi’ au ‘maonyi’.
Tarehe 20 Februari 2025, Profesa Choti Jonathan alipokumbana na neno ‘onesha’ katika makala yangu kuhusu kiambishi {ni}, alitoa maoni yafuatayo: Nafikiri umbo mwafaka ni onyesha bali si onesha kutokana na mabadiliko ya kifonolojia ambayo yanageuza [n] kuwa [ny].
Katika makala yajayo nitalitaja jibu langu kwa Profesa Choti pamoja na maoni niliyokuwa nimeyatoa mwaka wa 2014.
MAKALA YATAENDELEA