Habari za Kitaifa

Maandamano yalivyoweka Kenya kwenye hatari ya kunyimwa mikopo na mashirika ya kimataifa


HUENDA Kenya ikanyimwa mikopo baada ya kushushwa hadhi kwenye viwango vya Shirika la Kimataifa la kutathmini Madeni ya Mataifa na Utoaji Mikopo, Moody’s.

Ripoti ya Moody’s iliyotolewa Jumanne inaonyesha kuwa, kutotiwa saini kwa Mswada wa Fedha 2024/25 kumechangia Kenya kushuka viwango na kuwa kati ya nchi zinazoelekea kulemewa na madeni.

Kwa mujibu wa shirika hilo, inaonekana Kenya haitafanikiwa pakubwa kujiondoa hatarini hata katika mikakati ya kupunguza matumizi ya serikali.

Rais William Ruto aliondoa Mswada wa Fedha 2024 kutokana na wimbi la maandamano lililoshuhudiwa nchini kwa kuwa mapendekezo mengi ya ushuru yalikuwa katika mswada huo.

Kati ya sababu ambazo zilisababisha raia, hasa vijana wapinge mswada huo ni ushuru ambao ungeongezwa kwenye ununuzi na matumizi ya magari, kutuma na kutoa pesa na pia bei ya mkate kupanda maradufu.

Moody’s pia imeonya kuwa, huenda Kenya ikalemewa kuyalipa madeni yake na sasa imeorodheshwa miongoni mwa nchi hatari zaidi kupewa mikopo na mashirika ya kimataifa.

Mnamo Juni, shirika hilo lilitoa ripoti iliyoweka Ghana pabaya katika kuyalipa madeni yake. Nchi hiyo hatimaye ililemewa kabisa na sasa inashiriki mikakati ya kubana matumizi yake kulipa madeni mengi yanayoiandama.

Baada ya mswada wa fedha kuondolewa, serikali ya Kenya imeamua kupunguza malengo yake ya mapato ya ushuru mwaka wa fedha wa 2024/25 kwa Sh177 bilioni. Kando na hayo, pia imetangaza kuwa itapunguza matumizi katika afisi na idara mbalimbali za serikali kuanzia afisi ya Rais.

“Kushuka kwa nafasi ya Kenya kunaonyesha nchi haina uwezo wa kuyakusanya mapato ya kutosha ya kulipa madeni yake. Kwa hivyo, Kenya itakuwa ikitatizika sana kulipa madeni hayo kwa sababu ya kutaofikia mapato lengwa,” ikasema taarifa ya Shirika la Moody’s Jumanne.

Hasa shirika hilo lilisema kuwa, kupunguza matumizi hakutasaidia kwa sababu kiasi kikubwa cha ushuru kinaelekezwa katika kuyalipa madeni na hilo ni jambo ambalo haliwezi kuepukiwa kwa sasa.

“Serikali ya Kenya kwa sasa imepandishiwa gharama ya kupokea mikopo na kuwekewa masharti makali kabla ya kupewa mikopo,” ikaongeza taarifa hiyo.

Takwimu kutoka Benki Kuu ya Kenya zinaonyesha kuwa, deni la Kenya sasa limefikia Sh10 trilioni ambalo huchukua zaidi ya asilimia 70 ya mapato ya nchi.

Utawala wa Rais Ruto umekashifiwa kwa kuendelea kukopa fedha licha ya kiongozi wa nchi alipochukua usukani kusema alikuwa akilenga kukwepa mkondo wa kukopa kiholela.

Kwa muda wa miezi minane pekee baada ya kuchukua uongozi wa nchi, utawala wa Kenya Kwanza ulikopa Sh1.2 trilioni.

Katika mwaka wake wa kwanza baada ya kutwaa uongozi mnamo 2013, utawala wa Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ulikopa Sh874.5 bilioni.

Alipokuwa akiondoka afisini, Kenya ilikuwa na deni la Sh8.7 trilioni na ikilinganishwa na kiwango cha sasa cha Sh11.2 trilioni. Rais Ruto amekopa Sh2.5 trilioni ndani ya miaka miwili pekee ambayo amekuwa uongozini.

Deni la taifa limekuwa likisonga tangu 2013 kwa kuwa Rais wa tatu marehemu Mwai Kibaki alipoondoka afisini mnamo 2013, aliacha Kenya ikiwa na deni la Sh1.8 trilioni pekee.

Kwa mujibu wa data kutoka Benki Kuu (CBK) asilimia 73 ya deni la Kenya italipwa kwa Benki ya Dunia, Uchina, Benki ya AFB, Eurobond ambazo zinadai Kenya jumla ya Sh3.97 trilioni.

China ndiyo inadai Kenya hela nyingi zaidi ikiwa nchi hii ina deni lake la Sh1 trilioni.