Afya na Jamii

Jinsi ya kusafisha korodani na makosa yanayofanywa na wanaume

Na JACKSON NGARI August 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WANAUME wengi hawazingatii sana jinsi wanavyosafisha sehemu zao za siri. Wengi huamini kwamba kuoga kila siku kunatosha, lakini madaktari wa mfumo wa mkojo wanasema si kila wakati.

Kutumia sabuni kali, kukaa muda mrefu na chupi zenye jasho au kupuuza usafi wa sehemu za siri kunaweza kusababisha mwasho, fangasi, harufu mbaya na matatizo mengine yanayoweza kuzuiliwa.

Daktari mtaalamu wa mfumo wa mkojo, Dkt Victor Albert Okoth, anasema usafi wa korodani ni sehemu muhimu ya afya ya uzazi wa mwanaume.

“Usafi mzuri ni kusafisha sehemu hizo bila kupita kiasi. Ngozi ya sehemu za siri ni nyepesi na kuisugua sana kunaweza kusababisha majeraha na mwasho,” anasema.

Anashauri wanaume waoge sehemu za siri angalau mara moja kila siku kwa kutumia maji ya uvuguvugu.

Wakati wa kuoga, mwanaume anapaswa kuosha uume, korodani, kinena na eneo lililo kati ya korodani na njia ya haja kubwa.

Kwa wanaume ambao hawajatahiriwa, anashauri wavute govi nyuma, waoshe sehemu iliyo chini yake vizuri, wasuuze kwa maji kisha warudishe govi mahali pake.

“Hakuna haja ya kusugua korodani kwa nguvu. Tumia mikono. Kusudi ni kuondoa uchafu, si kuua kila kimelea,” anasema.

Dkt Okoth anaongeza kuwa wanaume wanaofanya mazoezi mara kwa mara, wanaofanya kazi nje au wanaokaa katika mazingira yenye joto wanapaswa kuoga tena baada ya kutoa jasho.

Anasema jasho hutengeneza mazingira yenye unyevunyevu yanayochochea ukuaji wa fangasi na bakteria.

“Hali ya hewa ya Kenya huwa na joto katika maeneo mengi. Kuoga baada ya mazoezi na kubadilisha chupi yenye jasho ni tabia muhimu ya kujikinga na maambukizi,” anasema.

Hata hivyo, anaonya kuwa kuosha sehemu hizo mara nyingi kupita kiasi kunaweza kuharibu kinga ya ngozi na kusababisha ukavu, mwasho na uvimbe.

Dkt Okoth anashauri matumizi ya maji pekee au sabuni laini isiyo na manukato makali.

Anasema wanaume wengi huamini sabuni zenye povu nyingi au harufu kali husafisha vizuri zaidi, jambo ambalo si kweli.

Bidhaa kama dawa za kuondoa harufu vinaweza kusababisha mwasho isipokuwa kwa ushauri wa daktari.

Baada ya kuoga, sehemu za siri zinapaswa kukaushwa vizuri kwa taulo safi.

Anasema unyevunyevu unaobaki kwenye ngozi huchochea ukuaji wa fangasi.

Kwa wanaume ambao hawajatahiriwa, sehemu iliyo chini ya govi inapaswa kukaushwa vizuri kabla ya kuirudisha.

Pia anashauri wanaume kuvaa chupi zinazopitisha hewa na kuzibadilisha kila siku au mara moja zinapolowa na jasho.

Dkt Okoth anasema makosa yanayofanywa mara nyingi ni kutosafisha chini ya govi, kutumia sabuni kali au manukato kwenye sehemu za siri, kuvaa chupi yenye jasho kwa muda mrefu na kunyoa nywele za sehemu za siri kwa ukali kiasi cha kujeruhi ngozi.

Anasema kosa kubwa zaidi ni kudhani kila tatizo la sehemu za siri husababishwa na uchafu.

“Harufu, vipele, uvimbe au usaha si lazima vitokane na ukosefu wa usafi. Magonjwa ya zinaa kama kisonono huenezwa kupitia ngono na yanahitaji uchunguzi na matibabu ya kitaalamu,” anasema.