Kwa nini haupaswi kupuuza kiungulia cha mara kwa mara
CAROLINE Awino, mama wa watoto watatu kutoka Nairobi, anakumbuka vizuri jinsi alivyopuuzilia mbali dalili za kiungulia kwa muda mrefu.
Kila mara baada ya kula chakula kizito au wakati wa usiku, alihisi moto kifuani na koo kuungua.
Kwa wakati huo, aliamini ni hali ya kawaida ambayo huwapata watu wengi, hasa baada ya kula kupita kiasi au vyakula vyenye mafuta mengi.
“Nilidhani ni hali ya kawaida tu. Ningeenda kwa duka la dawa, nichukue dawa ya kupunguza asidi na hali ingetulia. Sikuwahi kufikiria kuna tatizo kubwa,” anasema Caroline.
Hata hivyo, hali ilipozidi kuwa ya mara kwa mara, alianza kugundua mabadiliko yasiyo ya kawaida mwilini mwake.
Kwanza ilikuwa ni maumivu ya mara kwa mara kifuani, kisha ikafuata hali ya chakula kuhisi kama kimekwama kooni.
Usiku, alianza kupata kikohozi kisichoisha na sauti yake ikawa nzito kwa muda mrefu.
“Nilianza kuhisi kuna jambo. Nilikuwa naogopa kula wakati mwingine kwa sababu ya maumivu na ile hisia ya chakula kukwama,” anaeleza.
Baada ya kumwona daktari, alipatikana na tatizo la chakula kutoka tumboni kurudi mdomoni, hali inayojulikana kitaalamu kama GERD.
Hapo ndipo alitambua kuwa kile alichokuwa akipuuza kwa muda mrefu kilikuwa tayari kimegeuka kuwa tatizo kubwa la kiafya.
Kulingana na Jarida la American College of Gastroenterology na National Institutes of Health, kiungulia hutokea pale ambapo aside kutoka tumboni hupanda na kuja kwenye umio (esophagus).
Data hiyo pia inaeleza kuwa zaidi ya watu milioni 60 nchini Amerika hupata kiungulia angalau mara moja kwa mwezi, huku takribani milioni 15 wakikipata kila siku.
Na ulimwenguni kote, hali ya GERD huathiri kati ya asilimia 13.3 hadi 15.4 ya watu.
Daktari Bethwel Libeya, mfamasia na mtaalamu wa mafunzo ya tiba jijini Nairobi, anakubaliana na Jarida la American College of Gastroenterology na National Institutes of Health.

Anasema kuwa hali hii husababisha mwasho unaojulikana kama kiungulia, ambao mara nyingi huja kama moto au maumivu kifuani.
“Kila mara asidi inapopanda kutoka tumboni hadi kwenye umio, husababisha mwasho. Mwili unaweza kuvumilia kwa muda, lakini ikitokea mara kwa mara, huanza kuharibu ukuta wa umio,” anafafanua.
Anaongeza kuwa watu wengi hupuuza hali hii kwa sababu ni ya kawaida, hasa baada ya kula chakula kingi au chenye mafuta mengi.
Wengine hutegemea dawa za kupunguza asidi bila kufikiria chanzo cha tatizo.
“Tatizo ni pale kiungulia kinapokuwa mara kwa mara na kuanza kuathiri maisha ya kila siku. Hapo si hali ya kawaida tena, ni ishara ya tatizo kubwa kiafya,” anasema.
Kiungulia kisichotibiwa kwa muda mrefu kinaweza kusababisha madhara makubwa mwilini.
Wataalamu wanaeleza kuwa hali hii inapogeuka kuwa sugu, hujulikana kama GERD na inaweza kuleta athari mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuvimba kwa umio, vidonda, kutokwa na damu na hata kubana kwa umio.
Zaidi ya hayo, kuna hatari ya kupata ‘Barrett’s esophagus’, ambayo hubadilisha seli za umio na kuongeza uwezekano wa kupata saratani ya umio.
Ingawa hatari hiyo si kubwa kwa kila mtu, wataalamu wanasisitiza kuwa ni jambo lisilopaswa kupuuzwa.
“Kinachoanza kama mwasho mdogo kinaweza kugeuka kuwa tatizo sugu. Ndiyo maana ni muhimu kuchukua hatua mapema,” anasema Dkt Libeya.
Dalili za hatari mara nyingi huanza polepole na wengi huzipuuza.
Mtu anaweza kuanza kwa kupata kiungulia mara moja moja, lakini kadri muda unavyopita, dalili huongezeka na kuwa mbaya zaidi.
Ugumu wa kumeza chakula ni mojawapo ya ishara kuu kuwa hali imezidi.
Wengine huhisi kama chakula kimekwama kooni au kwenye umio, hali inayoweza kuleta hofu na usumbufu mkubwa.
Maumivu wakati wa kumeza, kupungua uzito bila sababu, kikohozi cha mara kwa mara hasa usiku na mabadiliko ya sauti pia ni dalili muhimu zinazopaswa kuzingatiwa.
Dalili hizi zinaonyesha kuwa asidi imeanza kuathiri si tu umio bali pia maeneo mengine kama koo na njia ya hewa.
Caroline anakiri kuwa alipuuza baadhi ya dalili hizi kwa muda mrefu bila kujua madhara yake.
“Nilikuwa napata kikohozi usiku na sauti yangu ilikuwa inabadilika, lakini sikuona kama ni jambo la kutilia maanani. Nilijua baadaye kuwa hizo zilikuwa ishara muhimu ambazo nilipaswa kuchukulia kwa uzito,” anasema.
Wataalamu wanashauri kuwa mtu yeyote anayepata kiungulia zaidi ya mara mbili kwa wiki, anapaswa kumwona daktari kwa uchunguzi zaidi.
Hali kadhalika, mtu anayepata shida ya kumeza, kupungua uzito bila sababu au maumivu makali kifuani anapaswa kutafuta matibabu haraka.
Dkt Libeya anaonya kuwa maumivu ya kifua yanaweza kuchanganywa na dalili za mshtuko wa moyo, jambo ambalo linaweza kuwa hatari ikiwa mtu atachukulia kawaida.
“Ikiwa maumivu ya kifua yanaambatana na kizunguzungu au maumivu yanayosambaa hadi mkononi, ni muhimu kutafuta msaada wa dharura mara moja,” anasisitiza.
Sababu za kiungulia zinahusiana kwa kiasi kikubwa na mtindo wa maisha.
Vyakula vyenye mafuta mengi, pilipili nyingi, kahawa na chokoleti vinaweza kuchochea hali hii.
Pia, kula chakula kingi kwa wakati mmoja au kulala pindi tu unapomaliza kula huongeza uwezekano wa asidi kupanda kutoka tumboni hadi kwenye umio.
Uzito kupita kiasi na msongo wa mawazo pia huchangia kwa kiasi kikubwa.
Hali hizi huongeza shinikizo tumboni na kufanya iwe rahisi kwa asidi kusukumwa juu kuelekea umio.
Kwa Caroline, kufanya mabadiliko ya maisha kulikuwa hatua muhimu katika kudhibiti hali yake.

Ingawa haikuwa rahisi mwanzoni, alilazimika kubadili mtindo wake wa kula na maisha kwa ujumla.
“Ilibidi nipunguze vyakula vya mafuta na kahawa ambayo nilikuwa napenda sana. Pia nilijifunza kutolala pindi tu baada ya kula. Mwanzoni ilikuwa changamoto, lakini sasa ninaona tofauti kubwa,” anasema.
Wataalamu wanashauri kuwa kubadilisha lishe na mtindo wa maisha ni hatua muhimu katika kudhibiti kiungulia.
“Epuka vyakula vinavyochochea dalili na hakikisha unakula kwa kiasi,” anaongeza Dkt Libeya.
Kusubiri kwa saa kadhaa kabla ya kulala baada ya kula pia husaidia kupunguza hatari ya asidi kupanda.
Pia, kuinua sehemu ya kichwa cha kitanda wakati wa kulala kunaweza kusaidia kuzuia asidi kurudi juu.
Hii ni njia rahisi lakini yenye ufanisi kwa watu wengi wanaosumbuliwa na kiungulia cha usiku.
Kuhusu matumizi ya dawa, Dkt Libeya anaonya dhidi ya matumizi ya muda mrefu bila ushauri wa daktari.
“Dawa za kupunguza asidi zinaweza kusaidia kwa muda mfupi, lakini hazipaswi kuwa suluhisho la kudumu bila uchunguzi. Ukigundua unazitumia kila siku kwa zaidi ya wiki mbili, basi unahitaji kumwona daktari,” anasema.