Matumaini tele mbegu za kiume zikiundwa katika maabara
KWA miaka mingi, wanaume waliogunduliwa kuwa gumba kabisa wamekuwa wakikabiliwa na ukweli mchungu kwamba huenda wasiweze kupata watoto.
Hata hivyo, utafiti mpya umeibua matumaini mapya baada ya wanasayansi kufanikiwa kutengeneza seli za awali za mbegu za uzazi za kiume katika maabara kwa kutumia seli zilizotokana na damu ya binadamu.
Utafiti huo, uliochapishwa katika jarida la kisayansi la Cell Stem Cell na watafiti wa Chuo Kikuu cha Pennsylvania nchini Amerika, unaonyesha hatua kubwa katika juhudi za kutengeneza mbegu za uzazi nje ya mwili wa binadamu.
Ingawa mbegu hizo hazikufikia ukomavu kamili wa kurutubisha yai, watafiti wanasema wamefikia hatua ambayo haijawahi kufikiwa katika tafiti za binadamu.
Wataalamu walitumia seli zilizobadilishwa kutoka kwenye damu na kuzielekeza kuwa seli za mwanzo zinazoweza kukua na kuwa mbegu za uzazi.
Baadaye waliziweka katika mazingira yanayofanana na korodani ndogo maabarani, ambako ziliendelea kukua na kuonyesha shughuli za vinasaba zinazofanana kwa asilimia 97 na ukuaji wa kawaida wa mbegu za uzazi kwa binadamu.
Iwapo teknolojia hii itafanikiwa kukamilishwa, inaweza kuwapa matumaini wanaume wanaokabiliwa na ugumba usiotibika kupata watoto wao kuzaa kwa kutumia mbegu zilizotengenezwa maabarani.
Ugumba wa wanaume ni tatizo kubwa duniani lakini mara nyingi huzungumziwa kwa kiwango kidogo.
Kulingana na Shirika la Afya Duniani (WHO), mtu mmoja kati ya sita hukumbwa na changamoto hili katika kipindi cha maisha yake ya uzazi.
Takriban asilimia 20 hadi 30 ya visa hivyo husababishwa na matatizo ya mwanaume pekee, huku katika asilimia 30 hadi 40 matatizo ya mwanaume na mwanamke yakichangia kwa pamoja.
Nchini Kenya, Chama cha Madaktari wataalamu wa Mfumo wa Mkojo kinasema kati ya asilimia 10 na 15 ya wanandoa hushindwa kupata watoto, na katika asilimia 60 ya visa hivyo tatizo huwa linahusu mwanaume kwa kiwango fulani au kikamilifu.
Mojawapo ya hali ngumu zaidi ni ile ambapo mwanaume hukosa mbegu za uzazi.
Kuna aina mbili za hali hiyo.
Ya kwanza hutokana na kuziba kwa njia za kupitisha mbegu na mara nyingi inaweza kutibiwa kwa upasuaji na ya pili hutokea pale korodani zinaposhindwa kabisa kuzalisha mbegu za uzazi, jambo ambalo lina tiba chache na ndilo lililolengwa na watafiti katika utafiti huu.
Kwa sasa, wanaume wengi wenye tatizo hilo hulazimika kufanyiwa upasuaji wa kutafuta mbegu za uzazi moja kwa moja kwenye korodani.
Hata hivyo, katika baadhi ya wagonjwa nafasi ya kupata hata mbegu moja inayoweza kutumika ni karibu asilimia 40 pekee.
Zaidi ya hayo, matibabu hayo pamoja hugharimu kati ya Sh150,000 na zaidi ya Sh500,000 kwa mzunguko mmoja nchini Kenya.
Gharama hizi hazifadhiliwi na Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA).
Katika utafiti huo, seli hizo ziliendelea kukua hadi hatua ambayo ni seli za mwanzo kabisa zinazozalisha mbegu za uzazi.
Hata hivyo, hazikufikia hatua ya mwisho ya kuwa mbegu kamili zinazoweza kurutubisha yai.
Kiongozi wa utafiti huo, Dkt Kotaro Sasaki wa Chuo Kikuu cha Pennsylvania, alisema tofauti kati ya seli za binadamu na zile za panya zilizotumika kusaidia ukuaji huenda ndiyo iliyozuia kukamilika kwa mchakato huo.
Hatua inayofuata ni kutumia seli zinazotokana na binadamu badala ya panya ili kuona kama mbegu kamili zinaweza kutengenezwa.