Afya na Jamii

Hizi hapa athari zinazoweza kutokea tohara isipofanywa kwa njia salama

Na PAULINE OGANJI October 24th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

MIAKA minne iliyopita, Bi Mary*, alimpeleka mwanawe wa miaka 11, Brian*, katika kliniki ya karibu ili atahiriwe.

Kama akina mama wengi katika eneo la Nyando, alijua kuwa tohara ilikuwa sehemu ya mpango mkubwa wa taifa wa kupambana na maambukizi ya virusi vya HIV.

Lakini hakuwahi kufikiria kuwa siku hiyo ingeishia kuwa mwanzo wa maumivu kwa mtoto wake.Miezi kadhaa baada ya upasuaji huo, Brian alianza kuugua. “Alianza kupata maumivu makali ya sehemu zake za siri, ikafuatwa na maambukizi ambayo hayakutibika kwa dawa za kawaida.”

Hatimaye, aligundulika kuwa na nasuri (fistula) ya uume, hali ambayo mara nyingi huhusishwa na wanawake baada ya kujifungua, lakini sasa inaonekana kuathiri wavulana wachanga kutokana na tohara zisizotekelezwa kwa viwango vya kitaalamu.

Kwa muda mrefu, tohara ya wanaume imekuwa ikihusishwa na manufaa ya kiafya, ikiwemo kupunguza uwezekano wa maambukizi ya HIV. Mwaka wa 2008, mpango wa hiari wa tohara kwa wanaume ulianzishwa rasmi chini ya ufadhili wa PEPFAR, na ulitekelezwa katika zaidi ya nchi 15 barani Afrika, zikiwemo Kenya, Uganda, Malawi, na Afrika Kusini.

Tangu wakati huo, zaidi ya wanaume milioni 15 walitahiriwa, 1.7 milioni kati yao nchini Kenya pekee.

Lakini baadaye, kulikuwa na uchunguzi kutokana na visa vya majeraha makubwa na maambukizi kuanza kuripotiwa, hasa miongoni mwa watoto wa chini ya miaka 15.

Ripoti iliyochapishwa Februari 12, 2021 na mashirika ya kimataifa ikiwemo CDC, WHO, USAID, na wengine, ilifichua kuwa visa 41 vya nasuri vilirekodiwa, visa vyote isipokuwa kimoja vikiwa ni miongoni mwa wavulana wa chini ya miaka 15.

Kulingana na Dkt Khisa Wakasiaka, mwanajinakolojia na mtaalam wa upasuaji wa nasuri, “Nasuri ni hali ya kiafya inayotokea pale ambapo tishu au ngozi katika sehemu za siri, hupata maambukizi au upungufu wa damu kiwango cha kuangamiza tishu.

Inaweza kusababisha harufu mbaya, maumivu makali, na hata kuhitaji upasuaji wa haraka ili kuondoa tishu zilizokufa.”
“Kwa kawaida, tunawaona wanawake wanaopata nasuri baada ya kujifungua, hasa katika maeneo yenye huduma duni za afya,” asema Dkt Khisa.

Lakini sasa, wavulana wachanga wanakumbwa na hali hii kutokana na tohara zisizofanywa kwa viwango vya usalama wa kimatibabu.
Uchambuzi wa visa hivi majuzi ulibaini kuwa wavulana kati ya miaka 10 hadi 11 walikuwa katika hatari zaidi.

Hii ni kwa sababu sehemu zao za siri bado ni changa, ngozi yao ni nyepesi, na miili yao haiwezi kustahimili maumivu au maambukizi kama mtu mzima.
Visa vingi vilitokea katika mazingira ya upasuaji yenye ukosefu wa vifaa vya kisasa, madaktari wasiohitimu vya kutosha, au uhaba wa dawa na huduma za dharura.

Katika baadhi ya matukio, watoto walitahiriwa bila ufuatiliaji wa kutosha, na hivyo maambukizi yakaendelea bila kugunduliwa mapema.

Kwa Brian, hali hiyo ilimlazimu kulazwa hospitalini kwa wiki kadhaa, na familia yake ilibeba mzigo mkubwa wa kifedha na kihisia. “Sikuweza kulala,” asema Bi Mary.

“Kila siku nilihisi kama nimechangia mateso ya mtoto wangu.”
Kwa sasa ni miaka minne baada ya Brian kupona, lakini mamake, Bi Mary anasema kwamba makovu yaliyotokana na maumivu ya mwanawe wakati huo, bado yangalipo.

Mwaka wa 2020, baada ya ripoti ya awali kuhusu majeraha, PEPFAR iliamua kusimamisha tohara kwa watoto wa chini ya miaka 15 katika nchi zote zinazotekeleza mradi huo.

Uamuzi huo uliungwa mkono na wanasayansi na madaktari waliohusika katika upelelezi.
Ripoti ya uchunguzi ilionyesha kuwa watoto 36 katika mataifa 15 walipoteza uume wao, kutokana na majeraha ya tohara. Takriban asilimia kubwa ya majeraha hayo yalitokea Kenya na Afrika Kusini.

Hata hivyo, PEPFAR ilieleza kuwa hatua hiyo inaweza kupitiwa upya, ikiwa nchi washirika zitathibitisha kuwepo kwa miundombinu madhubuti ya usalama, ufuatiliaji, na huduma ya dharura baada ya upasuaji.

Wataalamu wanakubaliana kuwa kwa kweli tohara kwa wanaume ni muhimu. Tohara ya hiari ni moja ya mikakati iliyopendekezwa na WHO kama njia mojawapo ya kudhibiti maambukizi ya HIV, kwa kuwa inaaminika kupunguza hatari ya maambukizi kwa wanaume.
Lakini pia wataalam wanatoa wito wa kuwepo na marekebisho wa mfumo wa utekelezaji wa tohara. Wanasema kwamba lazima kila upasuaji ufanywe na mtaalamu aliyehitimu, katika mazingira salama, na kwa vifaa vinavyofaa.

Aidha, kuna pendekezo la kuhakikisha wazazi wanapata taarifa sahihi kabla ya kuruhusu watoto wao kutahiriwa, pamoja na huduma ya ufuatiliaji wa afya ya mtoto kwa wiki kadhaa baada ya upasuaji.

Kenya haina takwimu za kutosha kuhusu visa vya nasuri ya uume miongoni mwa wavulana wadogo, vinavyotokana na madhara ya tohara.
Tafiti za kimataifa zinaonyesha kuwa visa hivyo huwatokea zaidi watoto walio chini ya umri wa miaka 15, hasa pale tohara inapofanywa na wahudumu wasiofunzwa au wa jadi.

Ripoti moja ilionyesha kuwa asilimia 98 ya visa vya nasuri ya umme vilitokea kwa wavulana chini ya miaka 15, jambo linaloonyesha hatari kubwa kwa kundi hili.

Ingawa kuna taarifa za madhara ya tohara kwa ujumla nchini Kenya, hakuna takwimu dhahiri kuhusu visa vya maradhi haya, na madhara mengi yanaweza yasiripotiwe hasa yakitokea nje ya vituo vya afya.

Ukosefu wa takwimu sahihi unaleta changamoto katika kuzuia na kushughulikia madhara haya.
Wataalamu wa afya wanapendekeza kuwepo kwa mfumo madhubuti wa kuripoti madhara ya tohara, kufuatilia visa vya nasuri ya uume, na kutoa mafunzo kwa wahudumu wote wa tohara ili kuzuia hali hizi.