Faida kiafya za pitaya na jinsi ya kuipanda
PITAYA, maarufu kama dragon fruit kwa Kiingereza, si tu tunda lenye rangi ya kuvutia, bali pia lina thamani kubwa kiafya.
Wataalamu wa lishe wanasema tunda hili ni chanzo kizuri cha vitamini C, ambayo huimarisha kinga ya mwili na kusaidia kupambana na magonjwa.
“Pia, lina vioksidishaji (antioxidants) vinavyosaidia kupunguza athari za sumu mwilini na kuchelewesha uzee wa seli,” anasema Diana Mureithi, mtaalamu wa masuala ya lishe katika serikali ya Kaunti ya Nairobi.
Mbali na hayo, pitaya ina virutubisho vya fiber vingi vinavyosaidia mmeng’enyo wa chakula (food digestion) na kuzuia matatizo kama vile haja kubwa kulemewa kutoka.
Diana anasema ni tunda lenye kiwango cha chini cha kalori, hivyo linafaa kwa watu wanaotaka kudhibiti uzito.
Hali kadhalika, lina madini kama chuma, magnesiamu na potasiamu, ambayo husaidia afya ya damu, mifupa na moyo.

Tunda hili pia lina maji kwa kiasi kikubwa, hivyo husaidia mwili kubaki na unyevunyevu.
Ulaji wa mara kwa mara unaweza kusaidia kupunguza hatari ya mardhi sugu kama kisukari na shinikizo la damu, hasa kutokana na uwezo wake kudhibiti sukari mwilini.
Kwa upande wa kilimo, dragon fruit ni mmea wa jamii ya cactus unaostahimili ukame, hivyo unafaa kwa maeneo kame na nusu-kame (ASAL).
Anthony Kinoti Mugambi ni mkulima anayezalisha pitaya Kathuura, Kiagu, Central Imenti, Kaunti ya Meru, eneo ambalo mvua ni nadra kushuhudiwa.
“Hukua vizuri katika udongo unaopitisha maji kwa urahisi, kwani maji mengi yanaweza kusababisha kuoza kwa mizizi,” Kinoti anaelezea.

Upandaji hufanywa kwa kutumia miche au vipandikizi (cuttings). Vipandikizi, Kinoti anasema huchukua kati ya mwaka mmoja hadi mwaka mmoja na nusu kuanza kuzaa.
Ni muhimu kuandaa shamba vizuri kwa kulainisha udongo na kuweka mbolea ya samadi ili kuongeza rutuba. Dragon fruit huhitaji miundombinu ya kuishikilia, kama nguzo za saruji au miti, kwa sababu hukua kwa kupanda juu.
Isitoshe, huhitaji mwanga wa kutosha wa jua ili kustawi na kutoa matunda mengi. Umwagiliaji maji unapaswa kuwa wa kiasi, hasa katika hatua za mwanzo za ukuaji.
Wakulima wanashauriwa kutumia mbolea za asili kama samadi ya ng’ombe, mbuzi au kondoo, huku mbolea ya kuku ikitumika zaidi wakati wa kuchana maua ili kuboresha mazao.