• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 6:17 PM
FATAKI: Si lazima kuzaa au kuolewa ndipo ukamilike kama mwanamke, usiishi kuridhisha waja

FATAKI: Si lazima kuzaa au kuolewa ndipo ukamilike kama mwanamke, usiishi kuridhisha waja

Na PAULINE ONGAJI

Kwa Muhtasari:

  • Maishani mwake hajawahi kuolewa ila alibahatika kukutana na dume la miaka 65 mtandaoni
  • Jamii imeweka viwango fulani kuhusu umri muafaka kwa mwanamke kuolewa
  • Ikiwa ndoto yako ni kusafiri duniani kote, basi usijinyime ili kuridhisha maoni ya watu

SIKU kadha zilizopita nilikuwa nikisafiri kuelekea nyumbani kutoka shughuli za kawaida katikati ya jiji la Nairobi.

Katika basi ambalo nilikuwa nimeabiri kulikuwa na mjadala uliokuwa unaendelea redioni ambapo watangazaji hao walikuwa wanazungumzia kuhusu binti ambaye alikuwa amepiga kueleza yanayomsibu.

“Nina miaka 52 na sijawahi olewa lakini nafurahi kutangaza kuwa nimebahatika kumpata mchumba ambaye napanga kufunga naye ndoa mwezi Julai,” alisema kwa furaha.

Kipusa huyo ambaye kulingana na sauti yake alionekana kuwa mrembo, maishani mwake hajawahi kuolewa ila alibahatika kukutana na kaka huyu mwenye umri wa miaka 65 kupitia mtandao wa kuunganisha wapenzi. Kwa mujibu wa binti huyu, mwanamume huyu alikuwa amejaribu ndoa mbili bila mafanikio.

“Miaka ilikuwa imepita kiasi cha kwamba watu walikuwa wananiambia kuwa hakuna matumaini ya kuolewa tena, lakini kwangu nilifahamu kuwa mwishowe ningepata mume,” alisema.

Ni hali ambayo utakubaliana nami kuwa imekuwa ikikumba mabinti wengi hasa wanapotimu umri fulani.

 

Umri wa kuolewa

Hii ni kwa sababu jamii imeweka viwango fulani kuhusu umri muafaka kwa mwanamke kuolewa. Kuna umri fulani maishani ambapo kama mwanamke unaanza kufanya watu kuingiwa na wasiwasi huku maswali ya lini utakapoolewa yakianza kuchipuka.

Wiki kadha zilizopita nilizungumzia taarifa fulani alizochapisha mtangazaji mmoja kuhusu jamii ilivyomkandamiza mwanamke huku ikiendelea kushusha thamani yake anavyozidi kuongeza umri tofauti na jinsi mwanamume husifiwa kwa uzuri wake anavyozidi kuzeeka.

Nakumbuka pia nikisisitiza kuwa huo ni upuuzi mtupu na ni uwongo ambao umeenezwa kwa muda mrefu kiasi cha kufanya wengi kuanza kuuamini.

Kuna binti fulani ambaye ni rafiki yangu kwenye mtandao wa Facebook ambaye siku kadha zilizopita alizungumza kuhusu jinsi amekuwa akipokea shinikizo kutoka kwa baadhi ya marafiki zake kupata mtoto huku wengi wakionekana kuhofia kwamba huenda akatalikiwa kabla ya kuafikia haya.

 

Ni lazima uzae?

Swali langu ni nani aliyesema kwamba ni lazima uzae ndio ukamilike kama mwanamke?

Nikidhani tuna muda mfupi sana ulimwenguni ambapo itakuwa muhimu kutumia wakati huo mchache kufanya jambo linalokufurahisha.

Ikiwa ndoto yako ni kuimarika katika taaluma na kusafiri duniani kote, basi usijinyime ili kuridhisha maoni ya watu. Na iwapo ndoto yako iko katika masuala ya mahusiano usiache kizingiti chochote hata iwe umri kikufungie njia.

Nakumbuka hadithi ya mwanamke wa miaka 92 kutoka Uganda ambaye hatimaye aliolewa baada ya kusubiri kwa miaka.

Kwa ufupi hakuna umri mkubwa zaidi unaomfungia mwanamke kuolewa. Ikiwa unahisi kuwa haujampata anayekufaa zaidi, zidi kutafuta bila haraka. Usiharakishe, kama wasemavyo wakati wa Mungu ndio mwafaka!

 

You can share this post!

Utafiti: Wasiotafuna mlo vyema hatarini kunenepa kupindukia

MAWAIDHA YA VALENTINE DEI: Uchu wa ngono si mapenzi kamwe!

adminleo