Hatima ya wanafunzi 3,500 Kerio Valley haijulikani walimu wakikimbilia usalama wao
HATIMA ya zaidi ya wanafunzi 3,500 Kerio Valley haijulikani huku walimu wasio wa eneo hilo wakiendelea kukwepa shule, wakihofia usalama wao kutokana na mauaji yanayotekelezwa na wahalifu waliojihami.
Licha ya serikali kuwahakikishia usalama, walimu wengi hasa wale waliopangisha nyumba wanakaa pembeni kwa sababu za kiusalama.
Usalama wa wanafunzi katika shule zilizo karibu na mipaka pia uko shakani, licha ya operesheni za usalama zinazoendelea.
Mauaji ya hivi majuzi ya mfanyakazi wa ujenzi, na mekanika na ule wa kasisi wa kanisa Katoliki yamezidisha hali hiyo.
Watu wengi wasio wenyeji wamekimbia mkoa huo, wakihofia kulengwa na wahalifu wenye silaha ambao wanawashuku kwa kufanya ujasusi na kutoa taarifa za kijasusi kwa mamlaka.
Baadhi ya walimu wasio wenyeji waliokimbia baada ya mashambulio ya hivi punde bado hawajarejea, hivyo kutatiza masomo katika zaidi ya shule 54 za msingi na 13 za upili, kulingana na Daniel Serem, katibu wa Chama cha Walimu Wakuu wa Shule za Msingi Kenya (Kepsha) Kaunti ya Elgeyo Marakwet.
“Tunapozungumza, baadhi ya walimu hawajaripoti shuleni mwao, na masomo yamekatizwa. Walimu wachache waliopo wanafanya kila wawezalo ili kuendeleza shughuli za masomo shuleni. Serikali imetuma maafisa wa usalama katika shule zilizoathirika ili kuimarisha usalama,” alisema.
Alibainisha kuwa shule zote za Kerio Valley zimefunguliwa isipokuwa Sekondari ya Tot, ambayo ilisalia kufungwa kufuatia mauaji ya kasisi huyo. Hata hivyo, uhaba wa walimu unaendelea kushuhudiwa.
Wiki jana, Kuppet na Knut waliwaagiza walimu katika eneo hilo kuacha kutoa huduma zao hadi usalama wao utakapohakikishwa.
Wakiongozwa na Katibu wa Kuppet Paul Biwott, viongozi wa vyama vya wafanyakazi walisema Ijumaa iliyopita hawataruhusu walimu kufanya kazi chini ya tishio la ghasia.
“Kwa sababu hiyo, shule zote za Kerio Valley zitasalia kufungwa hadi walimu wahakikishiwe usalama wao,” alisema Bw Biwott.
Katibu wa tawi la Marakwet Knut John Cketi na mwenzake wa Kuppet Biwott walithibitisha kuwa walimu wengi waliokuwa wametoroka wanasitasita kurejea.
“Licha ya serikali kuwahakikishia usalama, walimu wengi wasio wenyeji wanaogopa kurejea, hasa baada ya mauaji ya kasisi. Hakuna anayetaka kuhatarisha maisha yao,” alisema Bw Biwott.
Alisisitiza kwamba walimu na wanafunzi wana haki ya kulindwa na Serikali na hawatarudi shuleni hadi usalama wa kutosha utolewe.