Jamvi La Siasa

Jeshi jipya la kulinda kura za Ruto Mlimani

Na BENSON MATHEKA June 9th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

HUKU kiongozi wa chama cha Democratic Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua akiendelea kujijenga kutawala siasa katika eneo la Mlima Kenya, Rais William Ruto ameanza kuweka mikakati kupitia washirika wake wa karibu kukabiliana na uasi wa aliyekuwa naibu wake.

Katika hatua ya kimkakati, Dkt Ruto amewahusisha washirika wake waliobaki katika eneo la Mlima Kenya – Naibu wa Rais Prof Kithure Kindiki, Kiongozi wa Wengi Bungeni Kimani Ichung’wah, Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri na Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru.

Viongozi hawa wameanza kujitokeza waziwazi kumkabili Gachagua, huku wakimtetea Rais Ruto na sera zake, na pia kuonya dhidi ya siasa za mgawanyiko katika eneo hilo lenye ushawishi mkubwa wa kura.

Bw Ichung’wah ameongoza mashambulizi ya kisiasa dhidi ya Gachagua, akimtaja kama kiongozi anayehatarisha umoja wa eneo hilo kwa maslahi ya kibinafsi.

Akiwa mshirika wa karibu wa Rais Ruto, Ichung’wah amekuwa akisisitiza kuwa maendeleo ya eneo la Mlima Kenya hayawezi kupatikana kwa siasa za vitisho bali kwa ushirikiano na serikali kuu.

Mara si moja amewaongoza wabunge wa UDA kutoka eneo hilo kumshambulia Bw Gachagua.

Gavana Anne Waiguru naye amekuwa na msimamo thabiti wa kumtetea Rais Ruto na kueleza kuwa siasa za kuunda mirengo ndani ya Mlima Kenya hazifai.

Kama kiongozi mwanamke mwenye ushawishi mkubwa, amekuwa akihimiza ushirikiano kati ya viongozi wa eneo hilo na serikali kuu badala ya kuvuruga ajenda ya maendeleo kwa misingi ya kisiasa.

Waiguru pia ameonyesha dalili za kugombea kiti cha kitaifa katika uchaguzi mkuu ujao huku akimkosoa Bw Gachagua kwa kukemea viongozi wasiokubaliana naye.

Kiongozi wa Wengi Bungeni Kimani Ichung’wah

Katika kauli inayoonekana kulenga Gachagua na washirika wake katika eneo la Mlima Kenya, Bi Waiguru alionya wanaowadanganya wapigakura.

“Acheni kuzunguka mkidanganya watu, watu wetu wanafahamu mambo vizuri na hawawezi kudanganywa wala kushawishika kwa urahisi kupigia kura watu bila kuelewa,” Waiguru aliambia wakazi mapema wiki hii na kuongeza, “Siendi popote, bado nitakuwa kwenye siasa.”

Prof Kindiki, ambaye alimrithi Gachagua kama naibu wa rais amekuwa akiongoza kampeni kali ya kutetea serikali kupitia miradi ya maendeleo huku akizidisha mashambulizi dhidi ya wanaopinga utawala wa sasa.

Amekuwa akiahidi kuwa serikali itatimiza ahadi zake kwa wakazi wa eneo hilo. Ameungana na wenzake kumwaga pesa katika eneo hilo katika mpango wa unaoitwa uwezeshaji.

Mnamo Ijumaa, Naibu wa Rais alisema kuwa viongozi kutoka Mlima Kenya wanaomuunga mkono Rais Ruto watabaki serikalini kuhakikisha maendeleo yanawafikia wananchi waliowachagua akimlaumu Bw Gachagua kwa kuwa na tamaa.

“Sote tunajua kwamba yeye ni mwenye tamaa na anayejifikiria mwenyewe tu.

Anataka kuwaamuru viongozi wote wa eneo hili na kusukuma mbele maslahi yake binafsi tu, lazima ajifunze kuwaheshimu viongozi wengine. Hajui kila kitu.

“Tunataka viongozi wote washirikiane na wapewe muda wa kuwahudumia waliowachagua. Hatutaki kiongozi yeyote atishe kila mtu, hata wanamuziki. Acheni watu wafanye kazi,” alisema.

Bw Kiunjuri, mwanasiasa mwenye uzoefu wa siasa za Mlima Kenya, amejiunga na kundi hili la viongozi wanaompinga Gachagua.

Ameonya kuwa siasa za mirengo ndani ya eneo hilo zinahatarisha nafasi ya Mlima Kenya katika serikali ya kitaifa.

Kiunjuri amesisitiza kuwa ni lazima viongozi wote wawe na maono ya pamoja ya kuimarisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi badala ya kujihusisha na siasa za kugawanya eneo hilo.

Mnamo Alhamisi, alimshambulia Bw Gachagua akisema anajilazimisha kuwa msemaji wa eneo la Mlima.

“Sasa kwa kuwa ameunda chama chake, anataka kudhani kuwa yeye ndiye mtu mwenye maarifa kuliko wote, na viongozi wengine wa vyama kutoka eneo hili hawana busara kama yeye,” alisema Bw Kiunjuri.

Wadadisi wa siasa wanasema japo Gachagua anasisitiza eneo hilo lilimalizana na Rais Ruto na serikali yake alipotimuliwa serikalini mwaka jana na kwamba wakazi wengi wanahisi serikali haiwajibikii maslahi yao, washirika wa Rais Ruto katika eneo hilo wanajitahidi kuokoa jahazi.

“Washirika wa Ruto waliobaki katika Mlima Kenya na ambao hawaogopi kumtetea ni Prof Kindiki, Kiunjuri, Ichung’wah na Waiguru.

“Wengine wanaogopa hasira za wapigakura na ndio maana hawajitokezi kwa nguvu kama hawa wanne,” asema mchanganuzi wa siasa za Mlima Kenya Paul Kibe.

Anasema Rais anawatumia kujaribu kurejesha ushawishi uliomomonyoka kwa kasi baada ya kumbandua Gachagua ambaye ameungana na waliokuwa mawaziri Justin Muturi na Mithika Linturi kuongoza uasi eneo la Mlima Kenya.