Jamvi La Siasa

Wimbi jipya la DCP linavyotikisa Mlima

Na CHARLES WASONGA June 1st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

NAIBU RAIS Kithure Kindiki sasa anaonekana kufuata nyayo za mtangulizi wake Rigathi Gachagua kwa kufanya ziara nyingi katika ngome yake ya Mlima Kenya kwa ajili ya “kuirejesha serikalini”.

Mnamo Jumamosi wiki hii Profesa Kindiki kwa mara nyingine alizuru kaunti ya Embu ambapo aliwaonya maafisa wa serikali dhidi ya kujiingiza katika siasa.“Huu si wakati wa kuchapa siasa bali wa kuwatumikia wananchi.

Mkiniona hapa mjue kwamba nimekuja kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa niaba ya rais.

Kwa hivyo, maafisa wote wa serikali wanafaa kuiga mfano huu na kujitenga na siasa ili sote tutimize ajenda ya maendeleo ya serikali,” akaeleza alipohutubia umma Embu.

Alitumia fursa hiyo kumkaripia Bw Gachagua akimtaja kuwa mwanasiasa ambaye analenga “kuondoa serikalini” eneo la Mlima Kenya kupitia chama chake cha Democracy for Citizens Party (DCP).

Ziara hiyo ilikuwa ya 37 ambayo Profesa Kindiki amefanya katika eneo la Mlima Kenya mwezi Mei pekee.

Naibu Rais amezuru kaunti za Kiambu, Murang’a, Nyeri, Kirinyaga, Nyandarua, Laikipia akiongoza harambee za kuchanga fedha za kile kinachotajwa kuwa mpango wa serikali ya Kenya Kwanza kuwainua wafanyabiashara wadogo.Aidha, amekuwa akitembelewa na jumbe kadhaa kutoka kaunti hizo katika makazi yake rasmi Karen, Nairobi.

Katika mikutano hiyo ambayo huandaliwa na wandani wa Rais William Ruto kutoka Mlima Kenya, huchanga mamilioni ya pesa kutoka kwake na bosi wake, Dkt Ruto.

Wadadisi wa masuala ya siasa wanasema kuwa mikutano hiyo za kuchanga fedha za kuwapiga jeki wafanyabiashara wadogo ni mbinu mpya ambayo serikali, kupitia Profesa Kindiki, imeanzisha kuwavutia upande wake wakazi wa Mlima Kenya ambao wameikinai na kujiunga na mrengo wa Bw Gachagua.

“Hizi ni ziara za kisiasa. Anajaribu kuwabembeleza watu wa eneo hilo, haswa wafanyabiashara wadogo, wakulima wadogo na bodaboda waunge mkono serikali. Lakini hicho ni kibarua kigumu zaidi ikizingatiwa kuwa wimbi la chama cha DCP limeshika kasi katika eneo hilo,” anasema Gitile Naituli.

Hii ndiyo maana, kulingana na Profesa Naituli, Kindiki amekuwa akimsawiri Bw Gachagua ambaye ni kiongozi wa DCP kama anayeendeleza siasa za kikabila kwa kuunda chama anachodai kinaendeleza masilahi ya watu wa Mlima Kenya.

Juzi, akiendesha harambee katika eneo la Lari, Kiambu, Profesa Kindiki alidai kuwa Bw Gachagua analenga kugawanya nchi kuwili; sehemu moja iliyojikita katika siasa za kikabila na nyingine inayoendeleza siasa za maendeleo.

Mojawapo ya shtaka kwenye hoja ya kumtimua afisini kwa Bw Gachagua mwaka jana, lilikuwa kwamba aligeuza Afisa ya Naibu Rais kuwa afisi ya kuendeleza maslahi ya watu wa Mlima Kenya, badala ya kuhudumia taifa kwa ujumla.Hata hivyo, tofauti na Gachagua, Profesa Kindiki amekuwa akizuru maeneo mengine ya nchi kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo.

Kwa mfano mnamo Jumanne Naibu Rais alitua katika eneo la Kulamawe, kaunti ya Isiolo kukagua ujenzi wa barabara kuu kutoka Isiolo kuenda Mandera, yenye umbali wa kilomita 750.