Jinsi wanawake wanavyoasi pombe haramu na kukumbatia uhifadhi wa Misitu
Kwa miaka mingi, biashara ya pombe haramu imekuwa changamoto kubwa katika Kaunti ya Nandi.
Kulingana na wakazi wa eneo hilo, biashara hii imekuwa chanzo cha umaskini, kuzorota kwa afya, na mizozo ya kifamilia.
Ili kukwepa misako ya polisi, watengenezaji wamekuwa wakiendesha biashara hiyo kwa siri kwa kuficha pombe katika vichaka, mapango, kando ya mito, na misituni.
Hata hivyo, maafisa wa polisi wamekuwa kwenye mstari wa mbele kukabiliana nayo. Hivi karibuni, ripoti za polisi zilionyesha kuwa walifanikiwa kuharibu lita 5,000 za kangara zilizokuwa zimefichwa mapangoni, huku operesheni nyingine huko katika kata ndogo ya Kapkerer, Nandi South ikifanikisha uharibifu wa lita 3,010 za kangara na kukamatwa kwa lita 60 za chang’aa.
Baadhi ya wahusika wakuu kwenye biashara hiyo wamekuwa wanawake, waliokuwa wakiitengeneza na kuiuza kama njia ya kuchuma riziki ya kukidhi mahitaji ya familia zao.
Lakini kwa baadhi ya wanawake katika kaunti hiyo, simulizi imeanza kubadilika. Wameasi biashara hiyo haramu na kugeukia ukuzaji wa miche ya miti ya kiasili na matunda. Kwao, shughuli hiyo imekuwa njia ya kujichumia riziki huku wakichangia katika kurejesha misitu iliyoharibiwa.
Kulingana na Hellen Meli, uamuzi wa kuanza kukuza miche uliafikiwa baada ya kuachana na shughuli ya pombe iliyokuwa imeweka maisha yao hatarini.
“Tuliamua kuanza mradi huu kwa sababu tulikuwa tunatengeneza pombe aina ya chang’aa na tuliona haikuwa na manufaa kwetu. Ilikuwa inahatarisha maisha yetu kama wanawake wa Muruguiywet. Kama tungeendelea kutengeneza chang’aa na kukunywa, tungekuwa tumekufa kitambo.”
Kwa Meli, uzalishaji wa miche umewaletea mabadiliko makubwa. Shughuli hiyo imewaunganisha na kuwapa njia mbadala ya riziki. Fedha wanazozipata sasa zinawasaidia kugharamia mahitaji ya familia, ikiwemo elimu ya watoto wao.
“Tumependa mradi huu kwa sababu umetusaidia kwenye nyumba zetu. Watoto tumesomesha na tumenunua vitu vingi nyumbani kutokana na kazi hii.”
Mabadiliko hayo pia yameanza kupunguza utegemezi wa rasilimali za misitu, na hivyo kuchangia katika uhifadhi wa mazingira.
Hapo awali, baadhi ya wanawake walitegemea rasilimali za misitu kukidhi mahitaji yao ya kila siku. Walikuwa wakikata miti kwa ajili ya kuni na wakati mwingine kutumia maeneo ya misitu kuchunga mifugo yao, shughuli zilizochangia uharibifu wa misitu na maeneo yenye chemchemi.
Lakini kipato wanachopata kutokana na uzalishaji wa miche kimewawezesha kupata njia mbadala za nishati nyumbani.
Kulingana na Lucy Jepkemboi, baadhi ya wanawake wametumia mapato hayo kununua mitungi ya gesi, hatua ambayo imepunguza utegemezi wao wa kuni.
“Miche hii imetusaidia sana kwa maana kama kina mama, pesa tunazozipata tumeweza kununua mitungi ya gesi. Kwa sasa hatukati miti kutafuta kuni za kupikia, na hivyo tumeweza kuhifadhi mazingira.”
Kwa viongozi wa vikundi hivi, uhamasishaji wa jamii pamoja na ushirikiano na mashirika ya uhifadhi umeifanya jamii kuhusisha uhifadhi wa mazingira na shughuli zao za kila siku.
Kulingana na Jonah Lelei, Katibu wa kikundi cha SSG Muruguiywet, mradi huo ulianzishwa baada ya jamii kutambua kiwango cha uharibifu katika msitu wa Nandi North.
“Tulianza mradi huu kwa sababu tuliona uharibifu uliokuwa umefanyika ndani ya msitu wa Nandi North. Hivyo tukaja na lengo moja la kuhifadhi msitu. Mradi huu umesaidia kupunguza ujangili, ukataji wa miti, na uharibifu wa maeneo yenye chemchemi.”
Kwa Lelei, mradi huo haujawa tu chanzo cha kipato kwa wanawake, bali pia sehemu ya juhudi za jamii kulinda rasilimali za misitu.
Wanawake wameanza kuona thamani ya kuhifadhi msitu huku wakitafuta njia endelevu za kujipatia kipato.
Mtindo huu wa kukuza miche pia umezidi kuenea katika maeneo mengine ikiwemo Bonde la Ufa. Katika msitu wa Kessup, Kaunti ya Elgeyo Marakwet, wanawake wamejitwika jukumu la kurejesha misitu kwa kuzalisha miche ya miti ya kiasili.
Kufikia sasa, wamezalisha na kupanda takriban miche milioni moja na laki tano.
Kulingana na Florence Cherop, shughuli hiyo imewasaidia kujikimu, kujitegemea, na hata kutoa ajira kwa watu wengine katika jamii.
“Tunatumia rasilimali zetu kutoka nyumbani na tunawaajiri watu. Pia, miche hii imefanya tumejisajili na SHA, tunasomesha watoto wetu, na tunavaa kutokana na kazi hii.”
Kwa wanawake hao, vitalu vya miche vimekuwa zaidi ya shughuli ya uhifadhi; vimegeuka kuwa chanzo cha kipato kinachowasaidia kukidhi mahitaji ya familia zao.
Licha ya mafanikio hayo, wanawake hawa wanakabiliwa na changamoto zinazotishia ukuaji wa biashara zao. Mojawapo ya changamoto kubwa ni ukosefu wa soko la miche, licha ya kuwa na idadi kubwa ya miche iliyo tayari kupandwa.
Kulingana na Florence, kikundi chake kimekuza miche mingi lakini kinakosa wanunuzi na rasilimali za kutosha kuendeleza shughuli hiyo.
“Sasa tuko na miche zaidi ya milioni moja. Changamoto ni soko na hatuna pesa. Tunaomba mtusaidie ili watoto waende shule.”
Licha ya changamoto hiyo, Florence anasema wanawake hawajakata tamaa kwani mafanikio ya mradi huu yanategemea uvumilivu na juhudi za kutafuta masoko.
Mbali na ukosefu wa soko, uhaba wa maji kutokana na mabadiliko ya tabianchi ni pigo jingine.
Kulingana na Hellen Meli, ukame umeathiri ukuaji wa miche katika baadhi ya maeneo, huku uhaba wa mvua ukifanya iwe vigumu kupata maji ya kunyunyizia.
“Maeneo mbalimbali hayapati mvua kwa sababu haijapanda miti, na hii inachangia ukame. Wakati wa ukame tunakosa maji, jambo linalosababisha miche kukauka.”
Kutoka kwa kutengeneza na kuuza chang’aa hadi kuzalisha miche ya miti ya kiasili, safari ya wanawake hawa wa Nandi na Elgeyo Marakwet ni mfano wa kuigwa wa jinsi shughuli za kiuchumi zinavyoweza kuunganishwa na uhifadhi wa mazingira.
Hata hivyo, ili juhudi zao zisipotee bure, kuna haja ya haraka kwa serikali za kaunti, wadau wa mazingira, na mashirika ya kibinafsi kujitokeza na kusaidia kuunda masoko ya miche hii. Kwao, kila mche unaopandwa sio tu hatua ya kurejesha msitu, bali ni fursa ya kujenga maisha bora na yenye staha kwa familia zao.