Akili MaliMakala

Kenya inavyoweza kujiondoa kutoka kwa minyororo ya njaa

Na SAMMY WAWERU March 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MIFUMO ya umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa mifereji (irrigation) imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuimarisha usalama wa chakula na kuongeza uzalishaji wa kilimo, hasa wakati huu wa mabadiliko ya tabianchi.

Kenya, kulingana na Shirika la Chakula na Kilimo (FAO) la Umoja wa Mataifa (UN) ni miongoni mwa nchi zilizoathirika pakubwa na tabianchi Upembe wa Afrika.

Kulingana na Joshua Musyoka, meneja wa tawi la Plum Agri Irrigation, mfumo wa irrigation unaweza kupunguza athari za ukame na misukosuko ya hali ya hewa.

Anasema kuwa umwagiliaji, unyunyiziaji mimea na mashamba maji kwa kuutumia mifereji huhakikisha upatikanaji wa maji kwa usahihi na unaodhibitiwa, hivyo kupunguza uwezekano wa mazao kukauka mvua inapochelewa au kukosekana.

“Teknolojia za kisasa kama za kudondoa matone (drip irrigation), sprinklers na rain hose husambaza maji moja kwa moja kwenye mizizi ya mimea kwa ufanisi mkubwa,” anasema afisa huyo.

Hali hii huongeza kiwango cha mavuno, kuboresha ubora na kuruhusu uzalishaji wa mwaka mzima mfululizo badala ya kutegemea msimu mmoja wa mvua.

Joshua Musyoka, meneja wa tawi la Plum Agri Irrigation akielezea na kuonyesha mfumo wa irrigation kuzalisha chakula katika eneo kame kama vile Machakos. Picha|Sammy Waweru

Kupitia mafunzo na ushauri wa kitaalamu, Plum Agri Irrigation imesaidia zaidi ya wakulima 1,000 wa mashamba madogo na makubwa nchini kuwekeza kwenye mifumo inayolingana na mahitaji ya mashamba yao.

“Mwanzo, hutathmini hali ya shamba kabla ya kusimika mifereji ili kuzingatia chanzo cha maji, aina ya udongo, topografia na mazao yanayokusudiwa kulimwa. Huduma hutolewa kuanzia kwa upatikanaji wa vifaa bora, uwekaji, upimaji hadi ufuatiliaji wa utendakazi wa mifumo,” Musyoka anafafanua.

Hata hivyo, miradi mingi ya irrigation hufeli kwa sababu ya makosa yanayoweza kuepukika.

Musyoka kwenye mahojiano na Akilimali alisema changamoto kubwa ni usanifu duni usiozingatia upatikanaji wa maji, mahitaji ya zao au mwinuko wa ardhi.

Matumizi ya vifaa vya bei nafuu na visivyo na ubora, anasema husababisha kuvuja kwa mabomba, kuziba kwa mifereji na gharama kubwa za utengenezaji.

“Kukosa wataalamu wakati wa uwekaji au kujaribu kufanya kazi bila ujuzi wa kutosha hupunguza ufanisi wa mfumo wa irrigation,” anaonya.

Shamba lenye mfumo wa umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa mifereji, ndio irrigation. Picha|Sammy Waweru

Ili kuepuka hasara, wakulima wanapaswa kuanza na maandalizi sahihi ya shamba yanayoenda sambamba na mfumo uliochaguliwa.

“Ni muhimu kuchagua mabomba yenye ukubwa sahihi ili kusambaza maji kwa usawa na kufuata viwango vya maji vinavyohitajika kwa kila zao ili kuepuka unyunyiziaji kupita kiasi,” anashauri.

Ukaguzi wa mara kwa mara kutathmini uvujaji na kurekebisha husaidia kupunguza upotevu wa maji na gharama za uzalishaji.

Muhimu zaidi, kulingana na Musyoka ni kusaka ushauri wa kitaalamu wakati wa hatua za mwanzo, kuwekeza katika vifaa vya ubora wa hadhi ya juu na kuhudhuria mafunzo ya kilimo endelevu na jinsi ya kuangazia athari za tabianchi.

Anasisitiza ni muhimu kuepuka njia za mkato kwa kununua vifaa duni au kujaribu kusimika mfumo bila utaalamu.

Aidha, kununua mifumo kutoka kwa wasambazaji wanaoaminika badala ya madalali au mabroka na kuzingatia ubora, wakulima wanaweza kufanya irrigation kuwa mfumo endelevu, wenye faida na nguzo ya mapato ya muda mrefu licha ya kupanda kwa gharama za pembejeo.