Mtambo wa kisasa kuchoma maharagwe ya kahawa
KWA muda mrefu waongezaji kahawa thamani wamekuwa wakitumia mashine za kitambo kuchoma au kukaanga maharagwe ya kahawa.
Ni mojawapo ya hatua za kutamatisha ili kahawa kuwa tayari kugeuzwa kuwa kinywaji.
Hata hivyo, mashine za zamani zimeanza kupitwa na wakati za kisasa zikitawala sekta ya kilimo kufuatia kujiri kwa teknolojia na bunifu za kileo.
Kampuni ya Linkage Africa, inaunganisha, kutengeneza na kusambaza mtambo wa kisasa kuchoma kahawa – unaorahisisha huduma.

Kampuni hii yenye afisi zake Jijini Nairobi, ilitumia jukwaa la Maonyesho ya Kahawa mwaka huu, 2025, yaliyofanyika katika Taasisi ya Utafiti wa Kahawa (CRI) inayohudumu chini ya Shirika la Utafiti wa Kilimo na Mifugo Kenya (KALRO).
Yakiwa na kaulimbiu ‘Kuendeleza ubunifu wa kilimo kwa mifumo ya chakula yenye ustahimilivu na maisha endelevu,’ Linkage Africa ilihamasisha wakulima wa kahawa kuhusu modern coffee roaster machine.

Ni mashine ya kisasa kukaanga kahawa, ambayo, kulingana na Josphat Kyalo kutoka Linkage Africa, ni mtambo ulioundwa kwa matumizi ya kibiashara.
“Mashine hii ya kukaanga kahawa ya kibiashara ina mfumo wa kompyuta na huonyesha kiwango cha unyevuunyevu na joto la maharagwe ya kahawa,” Kyalo alieleza huku akionyesha jinsi mashine hiyo inavyofanya kazi.
Kukaanga au kuchoma, alisema mtambo huo unazalisha kilo 90 kwa kila saa.

“Hata hivyo, inaweza kurekebishwa ili kuzalisha zaidi,” Kyalo alisema.
Bei, inagharimu kima cha Sh2.6 milioni.
Maonyesho hayo ya kahawa ambayo yalikuwa Makala ya 19 yalifanyika katika makao makuu ya CRI, Ruiru, Kaunti ya Kiambu na yalileta pamoja wakulima kutoka maeneo yanayozalisha kahawa nchini, wadau kama vile kampuni za pembejeo, watafiti, wataalamu, wasindikaji, wauzaji, wasambazaji, na taasisi za kifedha.
