Makala

Teknolojia yazidi kuwa silaha muhimu katika kulinda biashara Afrika

Na WINNIE ONYANDO February 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

HUKU visa vya udukuzi wa mifumo ya kidijitali, wizi wa taarifa na ulaghai wa mtandaoni vikiendelea kuongezeka duniani, wataalamu wanasisitiza umuhimu wa kukumbatia mifumo ya kisasa ya kujilinda na kusimamia biashara na shughuli zao.

Kwa mujibu wa ripoti za sekta ya ICT, biashara nyingi barani Afrika bado zinategemea mifumo ya jadi ambayo huwa rahisi kudukuliwa au kusababisha hasara kutokana na ukosefu wa ufanisi.

Hali hii imeongeza hitaji la kukumbatia teknolojia ya kisasa zinazorahisisha usimamizi wa biashara, kuimarisha usalama wa taarifa na kuongeza uwazi wa miamala.

Ni katika muktadha huo ambapo kampuni kadhaa za teknolojia kutoka Afrika Mashariki zimeanza kupanua shughuli zao nje ya mipaka ya kitaifa.

Miongoni mwao ni Robisearch Limited, kampuni ya ICT yenye makao yake Kenya, ambayo mapema mwaka huu ilizindua tawi lake nchini Uganda kama sehemu ya mpango wa kupanua huduma zake za kidijitali kikanda.

Tawi hilo, lililopo Kampala, linakusudia kuhudumia wafanyabiashara wanaohitaji mifumo ya kidijitali ya kuendesha shughuli zao kwa ufanisi zaidi.

Nchini Kenya, kampuni hiyo imekuwa ikifanya kazi katika miji kadhaa ikiwemo Nairobi, Kisii na Mombasa, ikihudumia sekta kama biashara ndogo ndogo, mali na taasisi zinazotegemea mifumo ya mawasiliano na usimamizi.

Wachambuzi wa sekta wanasema biashara ndogo ndizo zilizo hatarini zaidi kukumbwa na hasara zinazotokana na ukosefu wa mifumo salama ya kidijitali.

“Biashara inayotumia mifumo ya kale iko kwenye hatari kubwa ya kuibiwa taarifa au fedha,” anasema Mkurugenzi wa Robisearch, kampuni ya kiteknolojia, Robert Manyala.

Mbali na Afrika Mashariki, kampuni hiyo inalenga masoko mengine barani Afrika, ikiwemo Afrika Kusini, ambapo kwa sasa huduma zake zinapatikana kwa njia ya mtandao huku mipango ya muda mrefu ikiendelea kutathminiwa.

Kadri uhalifu wa kidijitali unavyoongezeka, ndivyo umuhimu wa kukumbatia teknolojia salama, za kisasa na zinazoongeza ufanisi unavyozidi kuwa suala muhumi.