Akili MaliMakala

Uzinduzi wa kiwanda cha chakula cha mifugo kupunguza gharama

Na SAMMY WAWERU March 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KWA muda mrefu, sekta ya mifugo nchini imekuwa ikipitia changamoto kutokana na kuendelea kupanda kwa bei ya chakula. 

Hata hivyo, huenda ikapata afueni kutokana na kuzinduliwa kwa kiwanda kipya cha kisasa cha kuchakata chakula cha mifugo cha thamani ya Sh3 bilioni na kampuni ya Uholanzi ya malisho ya mifugo, De Heus.

Kiwanda hicho kilichoko Athi River, Kaunti ya Machakos kinatarajiwa kusaidia kukabiliana na upungufu mkubwa wa chakula kilichoafikia ubora, kuongeza uzalishaji, na kupunguza gharama kwa wafugaji, hasa kikilenga ufugaji wa ng’ombe wa maziwa, kuku, nguruwe na mifugo wengineo.

Kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha tani metri 240,000 ya chakula kwa mwaka — hatua muhimu kwa nchi inayokabiliwa na upungufu wa karibu tani metri 550,000 za chakula cha mifugo kila mwaka, kulingana na Idara ya Mifugo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi rasmi wiki iliyopita, Mwenyekiti wa Bodi ya De Heus, Co De Heus, alisema uwekezaji huo unaashiria imani ya muda mrefu katika sekta ya mifugo ya Kenya na kwa wakulima wake.

“Kiwanda hiki ni ishara ya imani tuliyonayo kwenye sekta ya ufugaji nchini Kenya na uwezo wake kiuzalishaji,” alisema De Heus.

Likiwa lilianzishwa mwaka 1911, shirika la De Heus limeimarika pakubwa na kuwa miongoni mwa kampuni zinazoongoza duniani katika uzalishaji chakula cha mifugo, ikiuza takribani tani milioni 16 za chakula, virutubisho na mchanganyiko maalum wa chakula kila mwaka kupitia zaidi ya viwanda 100 katika nchi 25.

Kiwanda cha Athi River kinaashiria kupanuka kwa shughuli zake barani Afrika, ambako De Heus inalenga kuzalisha zaidi ya tani milioni mbili za chakula miaka ijayo.

Kulingana na De Heus, kikifikia kilele chake cha kiwango cha uzalishaji kinaweza kuzalisha tani 20,000 kwa mwezi.

Mwenyekiti wa Bodi ya De Heus, Co De Heus wakati wa mahojiano na Akilimali eneo la Athi River, Machakos. Picha|Sammy Waweru

“Hii ni sawa na kilo milioni moja kwa siku — na kuhudumia maelfu ya wafugaji wa ng’ombe, kuku, mbuzi, kondoo, nguruwe, kati ya wanyama wengine wa nyumbani,” mwenyekiti huyo wa Bodi ya De Heus akaambia Akilimali kwenye mahojiano ya kipekee.

Inakadiriwa kuwa kiwanda hicho kitatoa ajira za moja kwa moja zipatazo 280, pamoja na nyingine nyingi zisizo za moja kwa moja kwenye mitandao ya usafirishaji, usambazaji na upatikanaji wa malighafi.

“Ununuzi wa malighafi, tutatangulia na yanayozalishwa nchini Kenya kama vile mahindi, soya, mabaki ya ngano na kanola. Hii itakuwa afueni kwa wakulima. Gapu itakayosalia, tutaagiza kutoka nje,” De Heus akaelezea.

Kenya, hata hivyo huagiza kutoka nje zaidi ya asilimia 70 ya malighafi yanayotumika kuunda chakula cha mifugo.

Licha ya serikali kuondoa kwa muda ushuru wa uagizaji mahindi ya manjano, soya, mbegu za pamba, mtama mweupe, unga wa samaki na alizeti, bei ya chakula cha mifugo imeendelea kuwa ghali.

Waziri wa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, Mutahi Kagwe, akiongea wakati wa uzinduzi wa kiwanda cha De Heus alisema uwekezaji huo ni wa kimikakati na unaowiana na azma ya serikali kuboresha sekta ya mifugo nchini. Alibainisha kuwa nchi inakabiliwa na upungufu mkubwa wa chakula cha mifugo, na sekta ya umma kwa ushirikiano na ile ya kibinafsi utasaidia kuleta afueni.

“Tuna upungufu wa zaidi ya asilimia 60 ya chakula cha mifugo, hali ambayo pia imechangiwa na athari za mabadiliko ya tabianchi kama vile ukame,” Waziri Kagwe akasema.

Uzinduzi wa De Heus, alisema utasaidia pakubwa kuboresha sekta kama vile ya uzalishaji maziwa nchini.

“Kenya inazalisha karibu lita bilioni 5.2 za maziwa kwa mwaka na tunalenga kufikia lita bilioni 10 hivi karibuni,” Kagwe alisema.

Alisisitiza kuwa lengo hilo litategemea lishe bora, virutubisho, afya ya mifugo na hasa chakula kilichoafikia ubora wa bidhaa.

Waziri wa Kilimo na Maendeleo ya Mifugo, Mutahi Kagwe, akizindua kiwanda cha De Heus. Picha|Sammy Waweru

Hali kadhalika, Waziri Kagwe alidokeza kwamba serikali inashughulikia mikakati kupunguza gharama ya uzalishaji wa chakula cha mifugo nchini, ikiwemo kusawazisha ushuru wa kaunti (cess) kusafirisha mazao ya kilimo, haswa usafirishaji mahindi na mabaki yake, kuhamasisha kilimo cha mihogo na soya, pamoja na kupunguza gharama za nishati na ushuru.

Kiwanda De Heus kina maabara ya kisasa yenye teknolojia ya Near Infrared (NIR) inayoweza kugundua sumu kama vile aflatoxin, huku malighafi yakipimwa kabla ya uzalishaji.

Balozi wa Uholanzi nchini Kenya, Hen Jan Bakker, alisema mradi huo unaonyesha ushirikiano dhabiti kwenye kilimo na ufugaji kati ya Kenya na Uholanzi.

Naye Gavana wa Machakos, Wavinya Ndeti, alielezea imani yake uwekezaji huo kusaidia kuimarisha kaunti hiyo hasa katika ukuzaji viwanda.

Mbali na uzalishaji, De Heus inapanga kuendesha mafunzo kwa wafugaji kote nchini kuhusu mifugo bora, makazi, umuhimu wa maji, udhibiti wa magonjwa, vimelea na jinsi ya kuwapa mifugo chakula — vigezo muhimu katika uongezaji uzalishaji.