Akili MaliMakala

Wanakuvunia na kukunywesha kahawa

Na SAMMY WAWERU June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

KARIBU miaka miwili iliyopita, wanachama wa Muungano wa Ushirika wa Wakulima wa Kahawa wa Ritho ulioko Gatundu Kusini, Kiambu, walipoamua kubadilisha mfumo wa uendeshaji biashara yao, hawakufahamu hatua hiyo ingewaletea mafanikio makubwa.

Ushirika huo ulioanzishwa 1995 ulianza shughuli za kuchakata kahawa Juni 2023, hatua ambayo sasa imewaletea faida wanachama.

“Ni miaka miwili sasa tangu tuzamie uongezaji thamani kahawa. Lengo letu ni kuhakikisha kahawa yetu inapatikana madukani kwa bei nafuu,” anasema Lucy Wambui, Meneja na Afisa Mkuu Mtendaji wa muungano huo wa Ushirika.

Lucy Wambui, Meneja na Afisa Mkuu Mtendaji Ritho Cooperative Society akipima kahawa kwenye ratili. Picha|Sammy Waweru

Ritho Farmers Cooperative Society Ltd (kwa Kiingereza) ina wanachama 2,000 wanaokuza kahawa eneo la Gatundu. Ingawa bado hawajaafikia kiwango cha juu cha uchakataji, tayari wameanza kunufaika na maamuzi yao.

Katika msimu wa 2023/2024, Wambui anadokeza kwamba wakulima walipelekea kiwanda cha ushirika huo kilo 970,000 za kahawa mbichi, hilo likiwa ongezeko kutoka kilo 795,000 msimu uliotangulia.

Kiwanda hicho ambacho pia hulima kahawa, msimu huo kilivuna kilo 5,000, kutoka kilo 3,000 – msimu uliotangulia.

Wambui anasema ongezeko hili linatokana na hamasa inayochochewa na uongezaji kahawa thamani. Kulingana naye, kuongeza kahawa thamani huwapa wakulima fursa ya kupata bei bora ya mazao.

Kahawa ya Ritho Cooperative ‘iliyochomwa’. Picha|Sammy Waweru

Ikiwa mpango wao wa uchakataji utatekelezwa kikamilifu, watakuwa na uwezo wa kudhibiti bei sokoni, tofauti na sasa ambapo wanategemea kwa kiasi kikubwa minada inayotegemea soko la kimataifa.

Ritho huchakata kahawa ya daraja la juu (premium) na ile ya kawaida, kupitia nembo ya yao ya Ritho Gold. “Tunataka pia kuendeleza utamaduni wa unywaji wa kahawa hapa nchini,” Wambui anasisitiza.

Mwenyekiti wa Ritho Farmers Cooperative Society Ltd, David Njoroge anakumbuka jinsi muungano huo wa ushirika 2016 ulivyolemewa na deni la Sh24 milioni, hali ambayo nusra iwasambaratishe.

“Tulikuwa tunakopa sana na wakulima hawakuwa wananufaika. Uamuzi wa kuanza uchakataji umebadilisha mambo na sasa wakulima wanapata mikopo bora na maisha yao yameimarika,” Njoroge akaambia Akilimali wakati wa mahojiano katika kiwanda cha Ritho.

Gredi tofauti za kahawa. Picha|Sammy Waweru

Kutokana na changamoto hizo, alisema wakulima wengi walikuwa wameanza kung’oa kahawa na kulima mazao mengine kama vile maparachichi, macadamia, au kuwekeza kwenye miradi ya ujenzi wa nyumba za kukodi.

Kuzamia uongezaji kahawa thamani, Wambui anafichua kwamba muungano huo wa ushirika uliuza baadhi ya vifaa vya zamani kama mashine ili kupata mtaji wa Sh900, 000 kununua mashine za kuchakata kahawa.

“Lakini mtaji mkubwa zaidi ulikuwa wakulima kujitolea kuunga mkono wazo la kuongeza kahawa thamani. Bila nia njema na makubaliano kutoka kwa wanachama, hatungefanikiwa,” Wambui anaeleza.

Maharagwe ya kahawa yanapofikishwa kiwandani hupitia hatua kadhaa kama vile kuondolewa maganda (hulling) – ambapo ganda la nje huondolewa. Kisha husafishwa, kupangwa kulingana na ukubwa na ubora kwa kutumia vichujio kabla ya kukaangwa na kusagwa.

Kando na kuongeza kahawa thamani, Ritho Cooperative hukuza zao hilo eneo la Gatundu, Kiambu. Picha|Sammy Waweru

Kiwanda cha uchakataji cha Ritho kina ukubwa wa futi 11 kwa 12, pia kina ofisi, sehemu ya kuhifadhia kahawa ambayo haijaondolewa maganda na kukaangwa, na maeneo mengine ya kazi.

Wanachama wa Ritho ndio wateja wao wa kwanza, huku pia wakiwa na duka mjini Gatundu kusambaza kahawa kwa wanunuzi wa nje.

Baadhi ya wateja huagiza kahawa kutoka nje ya nchi kupitia jamaa zao ambao ni wanachama. “Hii imefungua milango ya soko la kimataifa,” Wambui anasema.

Pia, wameanza kuhamasisha unywaji wa kahawa shuleni. “Lengo letu ni kulea kizazi kipya kinachokunywa kahawa. Hii itasaidia kuongeza mauzo na mapato,” anasema Njoroge, ambaye ni mwenyekiti wa Ritho Farmers Cooperative Society Ltd.

Mwenyekiti wa Ritho Farmers Cooperative Society Ltd, David Njoroge. Picha|Sammy Waweru

Pakiti ya gramu 250 ya Ritho Gold – ya hadhi ya juu, huuza Sh400, sawa na Sh1,600 kwa kilo, huku kahawa ya kawaida ikiuzwa Sh1, 200 kwa kilo. Kwa sasa wanachakata kilo 250 za kahawa ya daraja la juu kila mwezi. Wambui anafichua kuwa walipoanza, walikuwa wakichakata kilo tano pekee.

Afisa huyo anaamini, ikiwa wataongeza thamani kwa asilimia 40 hadi 50 ya kahawa yao, bei kwa mkulima itaongezeka hadi kufikia Sh150 kwa kilo.

Kenya huuza asilimia 95 ya kahawa yake nje ya nchi, huku asilimia tano pekee ikibaki kwa matumizi ya ndani kwa ndani. Hii ni ishara kuwa mtandao wa uongezaji kahawa thamani ukipanuliwa, sekta ya zao hili italetea wakulima faida chungu nzima.

Lucy Wambui, Meneja na Afisa Mkuu Mtendaji
Ritho Farmers Cooperative Society Ltd na mfanyakazi wakisaga kahawa kwenye kiwanda cha ushirika huo Gatundu, Kiambu. Picha|Sammy Waweru