Maoni

Gachagua akome kutusi viongozi, yeye si malaika!

Na CECIL ODONGO June 23rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KENYA ni taifa linalozingatia demokrasia ila tofauti za kisiasa hazifai kutumiwa na kiongozi mmoja kutusi wengine kana kwamba yeye ni malaika.

Siasa za matusi na chuki ambazo aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua anaendeleza ukanda wa Mlima Kenya hazifai hata kama nia yake ni kuwa kigogo wa siasa za eneo hilo.

Wikendi Bw Gachagua alikuwa katika mikutano ya kisiasa eneo la Meru ambapo kwa mara nyingine aliwarejelea wabunge wa eneo hilo kama ‘wajinga’ kutokana na ukuruba wao na Rais William Ruto.

Katika mkutano wa kisiasa mji wa Mikinduri eneobunge la Tigania Mashariki, Bw Gachagua alitumia matamshi makali dhidi ya mbunge wa eneo hilo Mpuru Aburi. Alidai mbunge huyo alikuwa amepanga njama ya kuvuruga au kutatiza mkutano wake lakini wananchi wakaishia kumlaki kishujaa.

Mwanzo, ghasia ambazo zilizingira mikutano ya Bw Gachagua zinastahili kulaaniwa kwa kinywa kipana kwa sababu katika nchi hii, kila kiongozi ana haki ya kuandaa mikutano na kutoa maoni yake kuhusu chochote kile.

Vilevile, hakuna kiongozi ambaye ni gwiji au mfalme wa fujo ndiposa mirengo yote ya kisiasa inastahili kuhakikisha kuwa amani inadumu.

Hata hivyo, hii tabia ya Bw Gachagua kuwatusi viongozi waliochaguliwa kwa sababu wanatofautiana naye kisiasa inapalilia chuki na huenda ndiyo sababu madai huzuka wamekuwa wakipanga fujo dhidi yake.

Wiki mbili alipokuwa katika Kaunti ya Kiambu, aliyekuwa naibu rais aliwatusi wabunge wa Mlima Kenya na kuwarejelea kama wajinga kwa sababu walitumiwa kumbandua mamlakani.

Na wikendi hii pia kando na kuendeleza matusi yake, pia aliwachochea raia wakwepe hoteli moja ambayo umiliki wake unahusishwa na Rais Ruto.

Hizi ni tabia za kitoto ambazo hazistahili kuvumiliwa kutoka kwa mtu aliyehudumu kama naibu kiongozi wa nchi.

Wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita, Bw Gachagua alikuwa na ushawishi katika siasa za Mlima na wengi wa wabunge hawa anaowatusi, alihusika katika kuwarai raia wawachague.

Aidha baada ya uchaguzi wa 2022, alishirikiana na wabunge hawa alipokuwa serikalini hasa kumpiga vita Kinara wa ODM Raila Odinga.

Hata baadhi ya sera za serikali zinazoonekana kuumiza raia kutokana na ushuru mwingi kama nyumba za gharama nafuu na Bima Mpya ya Afya (SHA) ziliasisiwa kama bado akiwa naibu rais na akawaambia wabunge hawa wapitishe.

Mara si moja akiwa serikalini, Bw Gachagua na wabunge hawa walikuwa wakiambia raia wavumilie ushuru wa juu kwa muda na nafuu itakuja kupitia miradi ya maendeleo.

Hata Bw Gachagua hakujitokeza hadharani kupinga mswada wa tata wa fedha wa 2024 ambao uliibua maandamano ya Gen Z mwaka jana. Alianza kuwa vuguvugu baada ya kuona mambo yanachacha.

Huyu sasa ndiye kiongozi anayewatusi wabunge na viongozi wengine waliochaguliwa eti ni wajinga?

Tofauti za kisiasa si ujinga na iwapo anaona wabunge kutoka mlima walio serikalini wanakosea kwa kutomfuata, kile anastahili kufanya ni kuwaambia raia wasiwachague tena badala ya kutumia lugha ya matusi.

Kinaya ni kuwa baadhi ya wabunge wanaotusiwa wana rekodi nzuri ya maendeleo hata kuliko aliyekuwa naibu rais na huenda anawaonea gere.

Ana haki ya kufanya kampeni na kuwa kigogo wa mlima lakini kukesha akiwatusi viongozi wenzake si ajenda ambayo itampaa umaarufu wowote nchini.