MAONI: Je, William Ruto ni Rais ‘bora zaidi’ ambaye Kenya huru imemkosa?
RAIS William Ruto amewahi kutoa kauli mbalimbali kuhusu uongozi wake anapojilinganisha na marais wa Kenya waliomtangulia.
Mnamo Septemba 12, 2025, Rais Ruto alijikomba: “Baadhi ya watangulizi wangu walikuwa wamekonga. Sijazeeka, ningali kijana. Nina tajriba ya kutosha. Nimekuwa mbunge kwa miaka 15. Nilikuwa naibu wa rais kwa miaka 10. Nimesoma sana. Huenda mimi ndiye rais aliyeelimika sana kuwahi kuchaguliwa Kenya.”
Marais watangulizi wa Ruto waliitumikia Kenya katika nyadhifa gani kabla ya kuwa marais? Michango yao katika kuiathiri sera ilikuwa ipi?
Nguvu na udhaifu wao ulikuwa upi? Rais Ruto alihudumu nyadhifa zipi chini ya watangulizi wake? Je, amekuwa katika ulingo wa siasa za Kenya kwa kipindi gani?
Maswali haya yatanisaidia kumkutadhaisha (contexualize) kauli ya Rais Ruto kwa minajili ya kuisaili na kuitathmini ili kubainisha iwapo ina mashiko, au la.
Tangu ijinyakulie uhuru mnamo 1963, Kenya imekuwa na marais watano. Rais wa sasa ni Ruto, ambaye amekuwa siasani kwa miaka 34. Safari yake katika siasa ilianza 1992 alipoanzisha vuguvugu la YK’92.
Jomo Kenyatta (1964–1978) alikuwa mwanaharakati na Mwanajumuiya ya Afrika (Pan -Africanist), Rais wa Kenya African National Union (KANU), na Waziri Mkuu wa kwanza – Kenya, (1963–1964).
Athari za kisera za Kenyatta zilionekana kupitia kwa wito wa Harambee, uliowarai wananchi kuungana katika ujenzi wa taifa.
Udhaifu wa Jomo Kenyatta ulikuwa ni ukandamizaji wa upinzani, na sera za ardhi zilizoyapembeza makabila mengine.
Kenyatta alipofariki 1978, Daniel arap Moi alishika hatamu za uongozi wa Kenya. Moi alikuwa mwalimu,mwanachama wa Legislative Council (LegCo), Waziri wa Masuala ya Ndani (1964 -1967), na makamu wa rais (1967 -1978).
Moi alifuata Nyayo za Kenyatta – akisisitiza ‘amani, upendo na umoja’. Alianzisha mfumo wa elimu wa 8-4-4- pamoja na kupanua elimu ya vyuo vikuu.
Moi aliimudu Kenya, licha ya misukosuko ya siasa za kijiografia (geopolitics) kipindi hicho.
Udhaifu wa Moi ulikuwa ni utawala wa kidikteta, ukiukaji wa haki za binadamu, ufisadi na uchumi uliodorora miaka ya 1990.
Ruto alihudumu kama Waziri wa Masuala ya Ndani mnamo 2002.
Mwai Kibaki alikuwa mhadhiri (Makerere), Waziri wa Fedha (1969 -1981), Makamu wa Rais (1978 -1988), na Kiongozi wa Upinzani (1998 -2002).
Sera yake iliyoibadilisha Kenya ni Mpango wa Elimu Bila Malipo mnamo 2003. Serikali ya Kibaki iliimarisha uchumi na miundombinu.
Ikiwa Rais Ruto alifanya kazi na marais wote – isipokuwa Jomo Kenyatta, mbona hakujifunza chochote kutoka kwa ubora na udhaifu wao?
Mbona hachoti tajriba zao kuiboresha Kenya kupindukia?
- Matundura ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Chuka