Habari za Kitaifa

Kang’ata ajiunga na Linda Mwananchi wiki chache baada ya kuhama UDA

Na FATUMA BARIKI June 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

GAVANA wa Murang’a Irungu Kang’ata kwa mara ya kwanza amejihusisha na kundi la Linda Mwananchi wiki kadha baada ya kugura chama tawala cha UDA.

Katika hatua inayotarajiwa kuibua gumzo kuu la kisiasa, Gavana Kang’ata alijiunga na kundi hilo wakati wa mkutano uliofanyika Kivulini, Thika, Juni 14, 2026.

Katika hotuba yake, Bw Kang’ata alisema amependezwa na maono ya Linda Mwananchi akisema vuguvugu hilo limebeba sura ya Kenya ya viongozi wachanga wasioongozwa na ukabila.

Aliiponda serikali ya Rais Ruto akisema sera zake zimekuwa na athari mbaya kwa wafanyabiashara na wanaviwanda.

“Hii serikali inaongeza ushuru kampuni ambazo zinatupatia kazi mpaka zinaondoka Thika, zinaondoka Mlima Kenya sababu ya gharama ya juu; na hivyo ndio vijana wanakosa kazi,” akasema Bw Kang’ata.

Alikosoa pia Ushuru wa Nyumba akisema fedha ambazo serikali inakusanya, alizodai zimefika Sh120 bilioni kufikia sasa, zingeelekezwa katika sekta ya elimu ili shule za kutwa ziwe bure kote nchini.

Alikashifu pia sera ya bima ya matibabu ya SHA akisema hospitali za Kaunti zinahangaika kutoa huduma kwa sababu serikali kupitia SHA hailipi madeni ya kusaidia huduma kuendelea.

Aliwataka viongozi wa Linda Mwananchi, Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino wamtafute aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ili kuunda upinzani thabiti utakaoweza kumng’oa Ruto mamlakani.

Bw Sifuna aliwaambia wafuasi kuwa Linda Mwananchi inajiandaa kwa kile alichokitaja kuwa mabadiliko makubwa ya kisiasa 2027, akimshutumu Rais Ruto kwa kushindwa kutekeleza ahadi alizotoa wakati wa kampeni za uchaguzi wa 2022.

“Watu wamechoshwa na ahadi zisizotekelezwa, gharama ya juu ya maisha na ukosefu wa ajira. Kama Linda Mwananchi, tuko tayari kushirikiana na viongozi wenye mawazo yanayofanana na yetu ili kuhakikisha mabadiliko yanapatikana 2027,” akasema.

Aliyekuwa Rais wa Chama cha Wanasheria Kenya (LSK), Faith Odhiambo, alitoa wito wa umoja wa kisiasa, akisema Wakenya wanapaswa kuunganisha juhudi zao ili kukomesha kile alichokitaja kuwa utawala mbovu.

Bw Owino aliwahimiza wapigakura kutokubali kushawishiwa na fedha wakati wa uchaguzi, akisema vijana ndio wanaobeba mzigo mkubwa wa ukosefu wa ajira na ugumu wa maisha ya kiuchumi.

Gavana wa Siaya, James Orengo, alisema eneo la Mlima Kenya linaendelea kuwa kitovu muhimu katika kuamua nani atakuwa rais wa Kenya, akidai kuwa Rais Ruto amepoteza uungwaji mkono katika maeneo kadhaa muhimu nchini.

“Suluhu za matatizo ya Kenya zitatoka eneo la Mlima Kenya. Rais amepoteza uungwaji mkono katika maeneo mbalimbali, ikiwemo Kisumu na Mombasa,” akasema Bw Orengo.

Mkutano huo ulitatizwa kwa muda na watu wanaoshukiwa kuwa wahuni, huku duru zikiarifu kuwa polisi wa eneo hilo walikuwa wameonywa dhidi ya kutoa ulinzi kwa hafla hiyo.

Kufikia wakati wa kuchapishwa kwa habari hii, Msemaji wa Polisi Michael Muchiri alikuwa bado hajajibu swali kuhusu madai hayo.