MAONI: Tuzoee kama nchi kukubali maoni na mitazamo kinzani
KADRI uchaguzi mkuu unavyojongea ndivyo tabia ya kufadhaisha isiyoruhusu mtazamo na msimamo tofauti inavyozidi kujitokeza.
Katika taifa linalojivunia demokrasia na utawala wa kikatiba, ungetarajia sote tunafahamu kila mwananchi, awe raia wa kawaida au kiongozi, amehakikishiwa kufurahia haki na uhuru kikatiba mradi hatoingilia uhuru na haki za mwananchi mwenzake.
Ni kinaya kuwaona watu mashuhuri walio mstari wa mbele ‘kutetea haki’ wakijihusisha na vitendo vya kusakama na kuwakandamiza raia wenzao.
Kuwaona wanasiasa wanaosimulia mara kwa mara masaibu waliyopitia watangulizi wao, wengine hata ikiwagharimu uhai wao, wakipigania demokrasia na mfumo wa vyama vingi, hii leo wakijaribu kuwanyamazisha wenzao kutoka kambi tofauti za kisiasa na wenye misimamo kinzani.
Tafran zilizozuka Homa Bay wikendi ambapo polisi na raia waliripotiwa kuuawa na kujeruhiwa ni mfano hai kuhusu tabia hii ya kijadi.
Kundi la viongozi lilipania kutoruhusu upinzani almaarufu Linda Mwananchi kufika eneo hilo wakisahau japo Homa Bay inachukuliwa kuwa ngome ya serikali pana, kuna Wakenya wanaounga mkono upinzani katika eneo lilo hilo sawia na ngome ‘za upinzani’ zinazosheheni wafuasi sugu wa serikali.
Isitoshe, demokrasia kikatiba inamhakikishia kila mwanasiasa na vyama vyote vya kisiasa haki ya kuendesha kampeni kwa njia ya amani na kuuza sera zao kwa raia kote nchini mradi tu uhuru huo unazingatia kanuni za sheria kuhusu kampeni.
Hali kwamba zaidi ya miaka 60 tangu Kenya ilipoanza kujitawala kidemokrasia bado kuna watu walioshikilia mawazo ya kijadi hususan kutumia vyombo vya dola kuzima maoni kinzani inashangaza mno.
Karamu ya kufana kuhusu harusi ya kitamaduni ya bintiye rais ni mfano mwingine.
Mkenya ambaye ni mwanahabari mashuhuri wa kimataifa alijipata mashakani vilevile, kosa lake pekee likiwa kuitikia mwaliko wa karamu ya kumwoza bintiye rais, huku watu wanaojitaja kuwa watetezi sugu wa haki za kibinadamu wakimkashifu vikali na kuwashawishi wafuasi wake mitandaoni kumtema.
Tukio hilo lililovutia hisia mseto pia lilifichua uhalisia wa kuhofisha kuhusu Wakenya wasiofanya maamuzi kibinafsi na badala yake wanafuata upepo wakipinga vikali au kuunga mkono upande au mwanasiasa fulani bila sababu thabiti.
Uhalisia ni kuwa, katiba ileile inayokupa uhuru wa kufahamishwa na kujieleza ikiwemo kwenye mitandao ya kijamii, ndiyo ileile inayomhakikishia mwingine kutangamana na kujihusisha na kiongozi au kambi yeyote kisiasa.
Wangari ni mwanahabari wa ‘Taifa Leo’