Kimataifa

Mundubile kupinga ushindi wa Hichilema mahakamani

Na REUTERS August 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

LUSAKA, Zambia:

KIONGOZI wa upinzani Zambia, Brian Mundubile, Alhamisi alisema atapinga matokeo ya uchaguzi wa urais uliofanyika Agosti 13 kortini, akidai kuwa kulikuwa na udanganyifu na ukiukaji mkubwa wa haki.

Mundubile alisema Jumatano jioni kuwa kampeni yake imekusanya ushahidi wa kasoro katika mchakato wa uchaguzi, kuhesabiwa kwa kura, kutumwa kwa matokeo na kutangazwa kwake.

“Kampeni yetu imeandika na kuhifadhi ushahidi wa ukiukaji mkubwa wa taratibu na kasoro zilizojitokeza katika mchakato wa uchaguzi,” alisema katika taarifa.

Mnamo Jumanne, Tume ya Uchaguzi ya Zambia ilimtangaza Rais Hakainde Hichilema mshindi baada ya kupata karibu asilimia 60 ya kura, huku Mundubile akipata asilimia 38.

Hata hivyo, ujumbe wa waangalizi wa Umoja wa Ulaya (EU) ulisema kulikuwa na masuala ya kutia wasiwasi kuhusu uwazi wa mchakato wa uchaguzi.

Waangalizi hao walidai wafanyakazi katika vituo vingi vya kupigia kura hawakuandika matokeo kwenye fomu rasmi mara moja baada ya kuyatangaza, kama inavyostahili kulingana na sheria.

“Katika karibu nusu ya maeneo tuliyotembelea, kulikuwa na mapumziko marefu wakati wa kujumuisha matokeo, huku maafisa wakionekana kusubiri maelekezo kutoka makao makuu kabla ya kutangaza matokeo,” ujumbe wa EU ulisema.

Tume ya uchaguzi ilisimamisha kuhesabu kura kwa saa kadhaa Ijumaa wiki jana kutokana na taarifa za vurugu dhidi ya maafisa wa uchaguzi na wizi wa karatasi za kura.

Baada ya uchaguzi, maafisa wa usalama waliwakamata watu 11, wakiwemo viongozi wa upinzani, katika oparesheni iliyohusisha makabiliano ya risasi.

Mundubile alitoa taarifa yake yake kuhusu hatua yake akiwa mahali pasipojulikana. Awali alisema alikuwa chini ya ulinzi kutokana na vitisho dhidi ya maisha yake.

Kamishina Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Kibinadamu, Volker Türk, amelaani kukamatwa kwa wanachama wa upinzani na kuitaka serikali kuheshimu haki za wote waliozuiliwa.