Michezo

Afisa wa Polisi ashinda Sh11 milioni Sportpesa Midweek Jackpot

Na CECIL ODONGO June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

Kutokana na uchumi mgumu unaoendelea kushuhudiwa nchini, wazazi wengi wamekuwa wakilemewa kumudu karo ya kuwasomesha watoto wao.

George Wasonga, 57 afisa wa polisi amekuwa na kibarua kuwalipia watoto wake karo chuoni. Kama mzazi amekuwa akijituma sana kuhakikisha wanatimiza kiu chao cha kupata elimu ya juu ili wajitegemee siku za baadaye.

Nuru ilimwaangazia Wasonga wiki hii baada ya dua yake kutimia na akashinda Sh11 milioni kwenye ubashiri wa  Sportpesa Midweek Jackpot.

“Nimekuwa nikipambana sana kuwasomesha watoto wangu na nia yangu imekuwa wasikose chochote maishani ili nao wawe na msingi wa kusaka kujizimbulia riziki siku zijazo,”akasema Wasonga, akiwa mwingi wa furaha baada ya kushinda hela hizo nyingi alizokiri zitasaidia kubadilisha maisha yake.

Alikuwa akiongea mtaa wa Shauri moyo viungani mwa jiji la Nairobi alipopokezwa hundi kutokana na ushindi wake ambao sasa unaashiria mwanzo wa ufanisi na maisha mazuri.

“Kupitia mapenzi ya mwenyezi Mungu sasa mambo yataimarika na wanangu watasoma na kufikia viwango vya juu vya elimu nchini. Sasa sina shaka kwa sababu kila kitu wanachohitaji, nitawatimizia,” akaongeza.

Kando na kuwasomesha wanawe, afande huyo tayari ameweka mikakati ya kupanua biashara zake kisha kufanyia nyumba yake ukarabati.

Wasonga amekuwa akibashiri mechi na Sportpesa tangu 2016 na amewahi kushinda  Sh15,000 mapema mwaka huu.

Hata baada ya kushinda Sh11 milioni  kuwahi bonasi ya 12 kwenye Mega Jackpots ameapa kuwa ataendelea kushiriki huku akilenga Mega Jackpot. Jumamosi hii Mega Jackpot ilikuwa imefika Sh420,655,592.

“Kwa wengine wanaobashiri jikazeni kwa sababu dua yenu itatimia. Nami nitaendelea kwa sababu nalenga fedha za juu zaidi kwenye Mega Jackpot,” akasema.