Bruno Fernandes apewa ofa mpya ya Sh11.3b kila mwaka akijiunga na Al-Hilal
NAHODHA Bruno Fernandes anaangalia kwa makini ofa nono kutoka kwa Al-Hilal itakayompa mshahara mara nne anapata kila mwaka kambini mwa Manchester United.
Kiungo huyo kutoka Ureno hupokea mshahara wa Sh2.7 bilioni kila mwaka ugani Old Trafford. Al-Hilal imeweka mezani mshahara wa Sh11.3 bilioni kila mwaka.
Taarifa zinasema kuwa ajenti wa Fernandes, Miguel Pinho, amefanya mazungumzo na Al-Hilal kuhusu kununuliwa kwa mchezaji huyo kwa Sh17.4 bilioni na United hawajakataa uwezekano wa kumuuza.
Iwapo uhamisho huo utafanyika, basi supastaa huyo atapanda kutoka nafasi 36-bora anakamata duniani wakati huu hadi nambari tatu duniani, nyuma ya washindi wa zamani wa tuzo ya Ballon d’Or Cristiano Ronaldo na Karim Benzema wanaokula Sh29.2 bilioni na Sh14.6 bilioni kambini mwa Al-Nassr na Al-Ittihad nchini Saudi Arabia, mtawalia.
United wanataka kuendelea kuwa na Fernandes, lakini wana presha ya kumuuza kutokana na kuwa wanapitia changamoto za kifedha na pia watakosa michuzi ya soka ya Bara Ulaya baada ya kukosa kufuzu.
Mashetani wekundu wa United walipigwa 1-0 na Tottenham Hotspur katika fainali ya Ligi ya Uropa ambayo ingewapa tiketi ya Klabu Bingwa Ulaya 2025-2026 na pia walimaliza Ligi Kuu ya Uingereza katika nafasi ya 15, nje sana ya maeneo sita-bora ya kushiriki mashindano ya Ulaya. Vilevile, vijana wa Ruben Amorim walibanduliwa na Fulham katika awamu ya 16-bora ya Kombe la FA ambalo washindi Crystal Palace walijikatia tiketi kushiriki Ligi ya Uropa msimu ujao.