Michezo

Kenya yajizolea medali 4 miereka ya Afrika nchini Misri

Na MWANDISHI WETU April 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TIMU ya Kenya ilianza vyema Mashindano ya Miereka ya Afrika jijini Alexandria, Misri, Jumatatu kwa kujinyakulia medali nne siku hiyo ya kwanza.

Ilipata fedha moja na shaba tatu, ishara ya mwanzo mzuri kwenye mashindano hayo yanayoendelea hadi Mei 2.

Jemimmah Nakhumicha alishinda fedha katika uzani wa kilo 65.

Wachezaji wengine watatu waliotwaa medali za shaba ni Joy Lichuma katika uzani wa kilo 57, Shaline Joy katika kilo 49, na Sophia Nancy katika uzani wa kilo 73.

Katibu Mkuu wa Chama cha Miereka ya Ridhaa nchini Kenya (KAWA), Eric Walucho, aliisifu timu hiyo akisema mafanikio hayo yanaonyesha maendeleo ya mchezo huo nchini.

Alieleza kuwa matokeo hayo ni habari njema kwa familia ya miereka, akimtukuza Mungu kwa ushindi huo.

Pia, alimpongeza Galfin Wangila kwa juhudi zake katika mtindo wa Greco-Roman uzani wa kilo 60, akisema “amefanya vyema sana, hongera.”

Nakhumicha na Lichuma walidhihirisha uthabiti kwa kushiriki katika uzani ule ule waliokuwa mwaka jana.

Shaline Joy alipanda kutoka kilo 45 hadi 49 na kufanya vizuri, huku Sophia Nancy akianza kwa kishindo mashindano ya Afrika kwa mara ya kwanza yake kwa kupata medali.

Wakenya walioratibiwa kuingia ulingoni jana ni Janet Ingwesi (kilo 69) katika kitengo cha kadeti cha wanawake.

Kwa upande wa wanaume, wawakilishi ni Calvin Nyatuka (kilo 65), Clinton Omari (kilo 51), Vincent Waweru (kilo 70), na Dan Kegode (kilo 60).

Kenya inalenga kuendeleza mawindo yake ya medali zaidi kadri mashindano yanavyoendelea.