• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 9:35 PM
Kisasi Kenya, UG zikionana katika mchujo wa raga

Kisasi Kenya, UG zikionana katika mchujo wa raga

Na GEOFFREY ANENE

KENYA na Uganda zitafufua uhasama wao kwenye raga wakati Lionesses itavaana na Lady Cranes katika mechi yao ya pili ya mashindano ya Afrika ya kufuzu kushiriki Kombe la Dunia la raga ya wachezaji 15 kila upande ya wanawake leo Jumanne mjini Johannesburg nchini Afrika Kusini.

Lionesses ilitoka chini mguso mmoja na kurarua Madagascar 35-5 katika mechi yake ya ufunguzi ilitosakatwa Agosti 9 nayo Uganda iliona cha mtema kuni dhidi ya Afrika Kusini ilipopepetwa 89-5 baadaye siku hiyo.

Kenya na Uganda zinafahamiana sana kutoka na kushiriki mashindano ya mataifa mawili ya Elgon Cup.

Tangu makala ya kwanza ya wanawake ya Elgon Cup mwaka 2006, majirani hawa wamekutana mara 18. Kenya inajivunia ushindi 11, Uganda imeshinda Kenya mara sita, huku mechi moja ikiishia sare.

Lionesses itaingia mchuano huu na motisha ya kutopoteza dhidi ya Lady Cranes katika mechi sita zilizopita. Mara ya mwisho mataifa haya yalikutana ni katika Elgon Cup mwaka 2019 pale Kenya ilikanyaga Uganda 44-13 Juni 22 mjini Kisumu na kuilima tena 35-5 Julai 13 jijini Kampala na kuhifadhi taji kwa mwaka wa tatu mfululizo.

Katika viwango bora vya raga duniani, Kenya inaorodheshwa katika nafasi ya 28 nayo Uganda iko nafasi 16 nyuma.

Baada ya kulima Madagascar, nahodha wa Kenya Philadelphia Olando alionya kuwa Lionesses inastahili kuimarika kabla ya kukutana na Uganda.

“Ilikuwa mechi ngumu kwetu mwanzoni kwa sababu Madagascar ilitubabaisha katika dakika 20 za kwanza. Hata hivyo, tulisalia watulivu katika uzuiaji wa mashambulizi na kuimarisha mashambulizi yetu, na hivyo ndivyo tulifaulu kurejea kwenye mechi na hatimaye kuishinda. Lazima turekebisha jinsi tunavyoanza mechi kwa sababu hatujafurahia jinsi tulicheza dhidi ya Madagascar katika dakika za mwanzo. Ni muhimu tuimarishe sehemu hii ya mchezo wetu kabla ya kurejea uwanjani,” alisema Olando, ambaye alichangia mguso mmoja katika mchuano huo, huku Celestine Masinde akipachika miguso miwili.

Kenya ilipata alama zake zingine kupitia kwa Janet Okelo, Diana Awino, Christabel Lindo (mguso mmoja kila mmoja), Janet Owino (penalti) na Irene Atieno (mkwaju).

Kulemewa

Kenya, ambayo mara ya mwisho ililemewa na Uganda ilikuwa 13-8 mwaka 2013 katika mechi ya marudiano ya Elgon Cup jijini Kampala, itajilaumu yenyewe ikidharau mahasimu hao wake.

Vyombo vya habari nchini Uganda vilinukuu kocha Edgar Lemerigar akiamini kuwa Lady Cranes inaweza kushangaza warembo wa kocha Felix Oloo. “Tulizidiwa maarifa na Afrika Kusini, lakini tunaweza kuchapa Kenya. Tunachohitaji tu kufanya ni kurekebisha makosa tuliyoyafanya dhidi ya Afrika Kusini,” alisema.

Mechi hii itasakatwa saa nane mchana. Itapisha mchuano kati ya Afrika Kusini na Madagascar. Raundi ya mwisho ya mechi za mchujo huu wa mataifa manne ni Agosti 17 wakati Uganda na Madagascar zitalimana saa nane, huku Kenya na Afrika Kusini zikikabiliana saa mbili baadaye.

Mshindi wa mashindano haya ataingia Kombe la Dunia mwaka 2021 nchini New Zealand. Nambari mbili atapata fursa ya mwisho ya kufika New Zealand kwa kumenyana na timu kutoka Amerika Kusini, Ulaya, Asia na Oceania.

You can share this post!

Wanaotumia majitaka kufanya kilimo Nairobi waonywa

KCB washinda Dala Sevens na kung’oa Mwamba kileleni

adminleo