Michezo

Mastercard yanogesha fainali ya UEFA

Na CECIL ODONGO June 1st, 2025 Kusoma ni dakika: 1

Mastercard Jumamosi usiku iliahidi kushirikiana na baadhi ya wanasoka bora Afrika na duniani kama njia ya kuhakikisha mashabiki wa soka Kenya wanatagusana na nguli wa mchezo huo.

Meneja wa Ukanda wa Afrika Mashariki na Visiwa vinavyopatikana Bahari Hindi Shehryar Ali alisema kuwa wana kibarua kikali kuhakikisha kuwa mchezo wa soka unakua kupitia ushirikiano na nguli hao wa soka.

“Soka ni mchezo ambao unapendwa sana na mashabiki Kenya wangependa sana kutangamana na wanasoka bora ili ndoto zao zitimie. Tutawaleta wanasoka bora Kenya ili kuwatia motisha mashabiki na wachezaji,” akasema Ali.

Alikuwa akiongea katika uwanja wa Carnivore mnamo Jumamosi usiku alipojumuika na mashabiki kutazama fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) kati ya PSG na Inter Milan. PSG ilishinda mchuano huo 5-0 na kutwaa ubingwa wake wa kwanza wa UEFA.  Mastercard ina mkataba wa ushirikiano wa miaka 30 na UEFA.

“Tunahitaji kuwaleta mastaa ili waje hapa na wawatie vijana wetu motisha ikizingatiwa kwa sasa Kenya inajaribu sana kuimarisha miundomsingi wake wa soka. Kupitia ushirikiano tunaweza kufanya kazi na washikadau wengine kukuza soka ya Kenya,” akaongeza Ali ambaye alikuwa akishabikia PSG kwenye fainali hiyo.

Jagina wa Nigeria Joseph Yobo alikuwa nyota wa kwanza kufika kwenye hafla ya kutazama fainali ya Uefa kupitia udhamini wa Mastercard miaka miwili iliyopita.

“Tunahitaji kushirikiana na washikadau kutoka sekta za umma na za kibinafsi  ili pia kuhakikisha talanta ya Kenya inapata nafasi nje hasa nchi zilizoendelea kwenye soka,

“Ningependa kumleta Achraf Hakimi ambaye anafanya vyema PSG hapa nchini na pia kumbuka kuwa Lionel Messi ni mmoja wa balozi wetu,” akasema.