Kimataifa

Rais Samia Suluhu ajikumbusha jinsi alikuwa mpishi hodari kwa mumewe  

Na WINNIE ONYANDO September 7th, 2024 1 min read

ILIKUWA video nadra sana na ya kipekee kumuona Rais wa Tanzania Mama Samia Suluhu akiwa jikoni akiandaa chakula.

Kwa kawaida, marais hawapiki chakula chao wenyewe, na hilo lilifanya video hiyo kuwa ya kipekee zaidi.

Akiwa amevalia aproni na kofia nyeupe, rais huyo wa kwanza mwanamke Afrika Mashariki alivutia makini ya mamia kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.

Kwenye video hiyo, Rais Samia alionekana akitumia mwiko kukoroga chakula alichokuwa akipika akiwa makini kabisa.

Video hiyo ilichukuliwa na Mariam, huku Rais akisema kwamba hajasahau kupika.

Alionekana akiweka ‘supu’ kiganjani kisha kuonja ikiwa chakula chenyewe kiko kimeiva sambamba.

“Tunaweza tukaonja na chumvi pia?” Mariam alimuuliza Rais Samia.

“Eeeh…wataka kuonja Mariam? Ngojea nionje mwenyewe niliyoweka kwanza. Bado sijaweka ndimu. Subiri,” Rais Samia alisema huku wakiangua kicheko.

Miongoni mwa waliovutiwa na video hiyo ni mwimbaji maarufu wa nyimbo za injili Christina Shusho, ambaye alionyesha kuvutiwa kwake kwenye ukurasa wake rasmi wa mtandao wa kijamii wa X (awali Twitter).

“Rais wangu anaweza kupika! Kwako kwa studio,” Shusho aliandika.

Rais Suluhu ambaye kwa sasa yuko nchini China kwa ajili ya mkutano wa tisa wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika ameoleka na ana watoto wanne.

Bintiye Wanu Hafidh Ameir, anafuata nyayo zake katika siasa na kwa sasa anahudumu kama mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.