• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 5:45 AM
JAMVI: Ishara The Service Party ndilo dau jipya la Ruto kuwania urais

JAMVI: Ishara The Service Party ndilo dau jipya la Ruto kuwania urais

Na WANDERI KAMAU

HATUA ya aliyekuwa Waziri wa Kilimo, Bw Mwangi Kiunjuri, kuzindua chama kipya cha The Service Party (TSP) Jumatano, imeibua maswali ya ikiwa ndicho “dau mbadala” kwa Naibu Rais William Ruto kuwania urais ielekeapo 2022.

Hili linatokana na mwonekano wa nembo na rangi za chama hicho na kauli yake kuwa hatawania ugavana katika Kaunti ya Laikipia.

Na ingawa kulikuwa na matarajio kuwa mwanasiasa huyo alikuwa na mipango ya kuzindua chama cha kisiasa, wadadisi wanasema kuwa kauli yake kuhusu kutowania ugavana ama nafasi yoyote kwenye uchaguzi wa 2022 inapaswa kutathminiwa kwa kina.

Chama hicho kina rangi za manjano na nyeusi, huku alama yake ikiwa moyo, kuonyesha upendo.

Vilevile, rangi zake zinafanana na zile za chama cha United Republican Party (URP) kilichokuwa chake Dkt Ruto, kabla ya kuungana na The National Alliance (TNA) cha Rais Uhuru Kenyatta kubuni muungano wa Jubilee mnamo 2012.

Kulingana na Bw Wycliffe Muga ambaye ni mchanganuzi wa siasa, uzinduzi wa chama hicho una nia fiche, ikizingatiwa kimezinduliwa wakati masaibu ya Dkt Ruto yanaendelea kuongezeka katika Chama cha Jubilee (JP).

Bw Kiunjuri ni mmojawapo wa washirika wakuu wa karibu wa kisiasa wa Dkt Ruto katika ukanda wa Mlima Kenya.

“Uzinduzi wa TSP si jambo la kawaida. Ni hatua yenye maana fiche kwa wanasiasa wanaojitayarisha kuwania urais ama uongozi wa Mlima Kenya kutoka kwa Rais Kenyatta. Bw Kiunjuri ni mwanasiasa mwenye tajriba kubwa, ikizingatiwa amekuwa siasani kwa zaidi ya miaka 15,” asema Bw Muga.

Na ijapokuwa Bw Kiunjuri hakufafanua undani kuhusu sababu kuu ya kuzinduliwa kwake, Bw Muga anaeleza kuwa huenda chama hicho kikawa “dau la kisiasa kuokoa jahazi ya Dkt Ruto ielekeapo 2022.”

Chama hicho kilizinduliwa siku moja baada ya mfanyabiashara Andrew Simiyu kuwasilisha nia ya kutaka kudumisha jina la chama cha Jubilee Asili.

Mwanzoni mwa wiki hii, Dkt Ruto alizindua kituo cha Jubilee Asili, washirika wake wa karibu kisiasa wakikitaja kama “eneo ambako watakuwa wakikutana kujadili mikakati ya Jubilee” baada ya ‘kufukuzwa’ kutoka makao makuu ya chama katika eneo la Pangani, Nairobi.

Ni hatua iliyozua midahalo kwenye majukwaa mbalimbali ya kisiasa nchini, baadhi ya wadadisi wakidai kuwa Dkt Ruto anajitayarisha kuzindua Chama cha Jubilee Asili.

Ni hilo linalotajwa kumshinikiza Bw Simiyu kwenda katika afisi za Msajili Mkuu wa Vyama vya Kisiasa, Bi Anne Nderitu kudumisha jina la chama hicho.

“Mienendo ya Dkt Ruto inafuatiliwa kwa ukaribu sana. Uwepo wa Bw Simiyu katika afisi za msajili wa vyama vya kisiasa kutaka kuhifadhi jina la Jubilee Asili unaashiria kivuli cha watu maarufu katika Jubilee, wanaodhani kuwa Dkt Ruto analenga kukitumia chama kuwania urais mnamo 2022. Hiyo huenda ikawa mojawapo ya sababu za Bw Kiunjuri kubuni TSP ‘kuwajibu’ wapinzani wa Dkt Ruto,” asema Bw Muga.

Bw Kiunjuri alifutwa kazi kama waziri na Rais Kenyatta mnamo Januari kwa madai ya kujihusisha kwenye siasa, licha ya mawaziri kuzuiwa na Katiba kujihusisha na masuala ya siasa.

Akiwa waziri, Bw Kiunjuri hakuwa akisita kuhudhuria mikutano iliyokuwa ikiandaliwa na wanasiasa wa mrengo wa ‘Tangatanga’ kutoka eneo la Mlima Kenya, wanaomuunga mkono Dkt Ruto.

Hajawahi kutupa marafiki

Na kwenye uzinduzi wa chama hicho, Bw Kiunjuri alisema kuwa tangu aanze siasa zake, hajawahi kuwatupa marafiki wake, ambapo si lengo lake kufanya hivyo hata baada ya kutoka serikalini.

“Urafiki ni nguzo muhimu sana kwenye siasa. Mimi ninafahamu umuhimu wa kudumisha urafiki na kuwakumbuka wenzako wanaokusaidia unapojipata pabaya,” akasema mwanasiasa huyo, bila kutoa ufafanuzi zaidi.

Ni kauli ambayo wadadisi wanafasiri kuwa dalili ya wazi mwanasiasa huyo yuko tayari kumpigania Dkt Ruto kwa hali na mali, hasa kutokana na masaibu ya kisiasa ambayo yanayomkumba katika JP.

Zaidi ya hayo, hilo linaonekana kama lawama fiche kwa Rais Kenyatta kwa kuendelea kumtenga Dkt Ruto kisiasa, licha ya kumsaidia sana kushinda urais mnamo 2013 na 2017.

“Bw Kiunjuri ni mwanasiasa anayesifkika kwa kuzungumza kwa mafumbo kuwasilisha jumbe zake. Uzunduzi wa chama hicho ni mojawapo ya jumbe anazowasilisha kwa mafumbo hayo,” asema Prof Ngugi Njoroge, ambaye ni mdadisi wa siasa.

Kumekuwa na uvumi kuwa mwanasiasa huyo huenda akawa mwaniaji-mwenza wa Dkt Ruto kwenye uchaguzi huo, ijapokuwa hajawahi kuzungumzia madai hayo hadharani.

Hii si mara yake ya kwanza kubuni chama cha kisiasa kwani mnamo 2012, alibuni chama cha The Grand National Unity (GNU) alichotumia kuwania ugavana katika Kaunti ya Laikipia mnamo 2013.

Na baada ya GNU ‘kumezwa’ na Jubilee mnamo 2017 Bw Kiunjuri anasema kuwa “hayuko tayari kurudia kosa hilo.”

Hata hivyo, baadhi ya wakosoaji wake wanataja hatua hiyo kama “iliyochelewa.”

You can share this post!

Pasta anaswa na mkewe kona mbaya

Wetang’ula aanza kujipigia debe mapema kumrithi Uhuru...

adminleo