UDA yaweka mchujo wa Ol Kalou Ijumaa kuepuka mvurugano na DCP
CHAMA cha United Democratic Alliance (UDA) kimebadilisha tarehe ya mchujo wa kuteua mgombea wa kiti cha ubunge wa Ol Kalou kutoka Jumamosi Mei 9 hadi Ijumaa Mei 8, hatua iliyowalazimu wawaniaji 10 kurekebisha mikakati yao ya kampeni.
Baadhi ya wawaniaji wamesema mabadiliko hayo yameathiri mipango yao ya mwisho ya kampeni.
Mwaniaji Ndung’u Wangenye, alisema ingawa hatua hiyo imeleta changamoto kisaikolojia kwa wafuasi wake, wako tayari kuafikiana kwa manufaa ya chama.
Naye Mary Nyokabi alieleza kuwa ratiba yake ya kampeni ilikuwa imepangwa hadi Ijumaa jioni, hivyo atalazimika kuibadilisha ili kuendana na hali mpya.
Hata hivyo, alikiri kuwa mabadiliko hayo yalitangazwa mapema na yanaweza kusaidia kuepuka changamoto iwapo uteuzi ungefanyika Jumamosi pamoja na shughuli nyingine za kisiasa.
Mwakilishi wa Wanawake Faith Gitau, anayesimamia kampeni za UDA, alisema mabadiliko hayo yalifanyika baada ya maombi na makubaliano ya wawaniaji wenyewe.
Mhandisi Peter Mugo pia aliunga mkono uamuzi huo, akisema wawaniaji wa UDA wako tayari kwa mchujo wa Ijumaa licha ya usumbufu uliosababishwa.
Mwakilishi wa Wanawake Faith Gitau, anayesimamia kampeni za UDA, alisema mabadiliko hayo yalifanyika baada ya maombi na makubaliano ya wawaniaji wenyewe.
Aliongeza kuwa chama sasa kinafanya haraka kuhakikisha maandalizi yote, ikiwemo vituo vya kupigia kura, yako tayari.
Mwenyekiti wa Bodi ya Uchaguzi ya UDA, Anthony Mwaura, alihakikishia umma kuwa zoezi hilo halitaathiri masomo shuleni.
Alisema wameomba kutumia madarasa yaliyo karibu na lango la shule ili kupunguza usumbufu, hasa ikizingatiwa kuwa muhula wa pili umeanza hivi majuzi.
Idadi kubwa ya wawaniaji imezua changamoto, hasa ikizingatiwa historia ya upigaji kura katika eneo hilo.
Wadi za Kanjuiri na Mirangine katika Kaunti Ndogo ya Mirangine kwa kawaida hupiga kura kama kambi moja yenye nguvu.
Ni kambi hiyo iliyomfanya aliyekuwa Mbunge wa Ol Kalou marehemu David Kiaraho bungeni.