• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 4:31 PM
Mukhisa Kituyi adaiwa kumdhulumu mwanamke kimapenzi

Mukhisa Kituyi adaiwa kumdhulumu mwanamke kimapenzi

WACHIRA MWANGI Na SAMMY WAWERU

MAAFISA wa Polisi Kaunti ya Mombasa katika kituo cha Nyali, wameanzisha uchunguzi wa kesi ya dhuluma inayomkabili aliyekuwa Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa Kuhusu Biashara na Maendeleo (UNCTAD), Dkt Mukhisa Kituyi.

Hii ni baada ya mwanamke mmoja kuwasilisha malalamishi akidai kudhulumiwa na mwanasiasa huyo ambaye ametangaza nia yake kuwania urais 2022.Hatua hiyo imejiri baada ya Inspekta Jeneral Mkuu wa Polisi, IG Hillary Mutyambai kuagiza mkuu wa polisi Ukanda wa Pwani, Paul Ndambuki kuanzisha uchunguzi kuhusu tetesi zinazomzingira Dkt Kituyi.

Bw Ndambuki ameiambia Taifa Leo Digitali, kwamba polisi wamekusanya taarifa ya mlalamishi – Bi Diana Opemi Lutta na ya mashahidi wengine watatu, ili kupata mwelekeo kumfungulia kesi ya mashtaka katibu huyo wa zamani UNCTAD.

“Tayari tumeanzisha kesi ya uchunguzi katika kituo cha polisi cha Nyali, ili tuwasilishe kesi hiyo katika Afisi ya Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka ya Umma (ODPP), atushauri iwapo uhalifu ulitekelezwa au la.

“Mlalamishi na mashahidi watatu wameandikisha taarifa. Mshtakiwa amearifiwa, na tunatarajia kuandikisha taarifa naye. Ameahidi kuwasilisha taarifa yake,” Bw Ndambuki akasema kwa njia ya simu.

Inasemekana Dkt Kituyi alimdhulumu Bi Lutta katika hoteli moja Mombasa, mnamo Mei 22, 2021, baada ya mlalamishi kukataa ombi lake kushiriki ngono.Kulingana na taarifa iliyoandikishwa katika kituo cha polisi cha Nyali, Lutta alidai kudhulumiwa na mchumba wake (Dkt Kituyi) katika hoteli ya Tamarind Village.

“Mshtakiwa alimsukuma (Bi Lutta) kutoka kitandani, akaanguka kwenye sakafu na baadaye kumgonga, akauguza jeraha katika mguu wake wa kushoto,” inaeleza taarifa ya polisi, iliyotazamwa na Taifa Leo Digitali.Bw Ndambuki amesisitiza kuwa uchunguzi unaendelea na kwamba kesi hiyo haijaondolewa kama ilivyoripotiwa na baadhi ya mitandao ya kijamii.

“Hatuna habari kuhusu kuondolewa kwa kesi hiyo. Kesi huondolewa wahusika, mlalamishi na mshtakiwa wanapokubaliana. Sina habari kuhusu madai hayo. Tunaendeleza malalamishi yenyewe jinsi yalivyo,” afisa huyo akasisitiza.

  • Tags

You can share this post!

TAHARIRI: Tumalize uhuni wa wanafunzi shuleni

Hatari ya Sagana River Water Fall, Muruguru – Nyeri