Habari za Kitaifa

Wandani wa Ruto Mlimani waweka presha Hassan Omar atimuliwe

Na COLLINS OMULO May 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SHINIKIZO zinaendelea kuongezeka kwa Katibu Mkuu wa chama cha United Democratic Alliance (UDA), Hassan Omar, kufuatia matamshi yake yanayodaiwa kuchochea chuki za kikabila, huku viongozi kadhaa wakitaka ajiuzulu au afurushwe kutoka wadhifa huo.

Mwanasiasa huyo ambaye aliwahi kujijengea jina kama mtetezi wa haki za binadamu sasa anakabiliwa na wakati mgumu kisiasa baada ya kauli zake kuzua mjadala mkali nchini.

Duru zinasema viongozi kutoka eneo la Mlima Kenya wanaomuunga mkono Rais William Ruto wanapanga kuwasilisha ombi rasmi kwa Rais wakimtaka kuchukua hatua kali dhidi ya Omar.

Viongozi hao tayari wamewasiliana na mwenyekiti wa UDA Cecily Mbarire pamoja na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Taifa Kimani Ichung’wah ili kufikisha msimamo wao kwa Rais.

Hasira dhidi ya Omar zimeendelea kuongezeka licha ya yeye kuomba msamaha na kusema matamshi yake yalitafsiriwa vibaya na kueleweka nje ya muktadha.

Alitoa kauli hizi wakati wa hafla ya kutoa hati za kumiliki ardhi iliyoongozwa na Rais William Ruto katika Kaunti ya Mombasa mwishoni mwa wiki.

Matamshi yake yalitafsiriwa na baadhi ya viongozi kama yaliyolenga jamii ya Mlima Kenya baada ya kumlaumu “baba mwanzilishi wa taifa na mwanawe” kwa madai ya kuhusika katika dhuluma za ardhi katika eneo la Pwani.

Omar pia alitoa wito wa kuchukuliwa hatua za kisheria dhidi ya wanaodaiwa kupora ardhi, akisema baadhi yao wanafaa kuwa gerezani.

Hata hivyo, viongozi wengi kutoka Mlima Kenya wamekataa ombi lake la msamaha wakisema kauli zake zilikuwa za makusudi zilizolenga kuchochea mgawanyiko wa kikabila.

Mbunge wa Mathira Eric Wamumbi alisema Omar hafai kuendelea kuwa Katibu Mkuu wa chama tawala kwa sababu nafasi hiyo inahitaji mtu anayewaunganisha Wakenya badala ya kuwagawanya.

“Tutamwandikia kiongozi wa chama pamoja na uongozi wa UDA ili aondolewe katika wadhifa huo. Viongozi wengine waliowahi kutoa matamshi yaliyokera wananchi walijiuzulu, na hivyo jambo la heshima kwa Hassan Omar ni kujiuzulu,” alisema Wamumbi.

Mbunge huyo alisema kauli za Omar zimewaweka viongozi wanaomuunga mkono Rais kutoka Mlima Kenya katika hali ngumu kisiasa.

“Rais hapaswi kulaumiwa kwa matamshi ya Hassan Omar. Yeye ndiye anapaswa kubeba mzigo wa kauli zake,” akaongeza.

Aliyekuwa Katibu Mkuu wa UDA na Seneta Maalum Veronica Maina alisema haiwezekani kwa Omar kuendelea kushikilia wadhifa huo.

“Ofisi ya Katibu Mkuu wa chama tawala inapaswa kuwa ishara ya matumaini, maridhiano na umoja wa taifa. Matamshi yake yako chini ya kiwango kinachotarajiwa,” alisema Maina.

Mwakilishi wa Kike wa Nyeri Rahab Mukami naye alisema viongozi kutoka Mlima Kenya wako tayari kuhakikisha Omar anaondolewa afisini iwapo ataendelea kutoa matamshi ya aina hiyo.

Wakati huo huo, Tume ya Uwiano na Utangamano wa Kitaifa (NCIC) imeanzisha hatua za kuchunguza matamshi hayo yanayodaiwa kuwa ya chuki.

Viongozi wa kidini pia wamejitokeza kulaani kauli hizo wakisema hazifai katika taifa linalotafuta umoja na mshikamano.

Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alisema viongozi wa Mlima Kenya hawatakubali msamaha wa Omar.

“Tunakataa kabisa jaribio la Hassan Omar kuomba msamaha kwa kuwachochea Wakenya dhidi ya watu wa Mlima Kenya,” alisema Gachagua.

Mwakilishi wa Kike wa Kirinyaga Njeri Maina alisema Omar alijua vyema kile alichokuwa akisema kwa sababu yeye si mgeni katika siasa.