Habari za Kitaifa

Madai yafichuka ya hujuma, mvutano katika kikosi cha kulinda Rais

Na KAMORE MAINA May 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KUTOAMINIANA na hujuma vilichochea mvutano ndani ya Kitengo cha Ulinzi wa Rais hali iliyosababisha mzozo kati ya maafisa wa polisi wa ngazi za chini na wakuu wao na hatimaye kuleta mapengo kadhaa ya kiusalama, imefahamika.

Kwa maafisa wa Ikulu na Inspekta Jenerali wa Polisi, tukio la Jumapili iliyopita katika Kaunti ya Kilifi ambapo mwanamume alifanikiwa kumfikia Rais William Ruto lilikuwa kilele cha taharuki, na ishara kuwa kitengo hicho kilihitaji uongozi mpya.

Uchunguzi na mahojiano na maafisa wa polisi unaonyesha kuwa, mazingira ya kazi yalikuwa ya sumu, huku baadhi ya maafisa wa chini wakilalamikia kunyanyaswa na wakuu wao na kupendelewa kwa kundi fulani, hasa katika mgao wa majukumu yanayoambatana na posho kubwa.

Mgawanyiko kati ya baadhi ya wakuu pia uliathiri maafisa wa chini, ambapo makundi mawili yalijikuta yakipeleleza wenzao ili kupata makosa yanayoweza kuwafanya wachukuliwe hatua.

Pia, kumekuwepo na malalamiko kuwa baadhi ya makamanda walikuwa wakizuia posho za maafisa wa chini wanaolinda Rais na Ikulu.

Aidha, maafisa wanadai baadhi ya wakuu wao walipendelea wazi wazi katika kuteua maafisa wanaosafiri na Rais katika ziara za nje ya nchi, jambo lililoongeza hali ya kutoridhika.