Kimataifa

Tinubu aagiza maafisa wafanye halahala kuokoa wanafunzi waliotekwa nyara

March 14th, 2024 2 min read

NA MASHIRIKA

ABUJA, NIGERIA

RAIS wa Nigeria Bola Tinubu ameamuru maafisa wa usalama kutolipa ridhaa kwa ajili ya kuachiliwa kwa zaidi ya wanafunzi 250 wa shule ya msingi waliotekwa nyara na watu waliojihami kwa silaha wiki iliyopita, Waziri wa Habari amesema Jumatano.

Familia za wanafunzi hao zinasema watekaji nyara wanaitisha ridhaa kubwa ili kuwaachilia.

Waathiriwa walitekwa nyara shuleni mnamo Alhamisi wiki jana katika kijiji cha Kuriga kilichoko Kaskazini Magharibi mwa jimbo la Kaduna.

Magenge ya wahalifu mara nyingi huteka nyara watu wengi kaskazini mwa Nigeria, yakilenga shule, vijiji na barabara kuu.

Katika miaka mitatu iliyopita, mamia ya wanafunzi walitekwa nyara.

Waathiriwa wa utekaji nyara nchini Nigeria mara nyingi huachiwa huru baada ya kufanya mazungumzo na serikali, ingawa maafisa wanakanusha malipo ya fidia kufanyika.

Kwa kuzingatia msimamo rasmi wa serikali, waziri Mohammed Idris alisema Rais Tinubu aliwaambia maafisa wa usalama wanaowatafuta wanafunzi kuhakikisha “hakuna hata senti moja inayolipwa”.

Kadhalika, alisema kufuatia agizo la Rais Tinubu, shughuli ya kuokoa watoto hao ni ya dharura na kuongeza kwamba waliamrishwa na kiongozi wa nchi kuhakikisha kila mtoto aliyetekwa nyara anaokolewa na kurudishwa nyumbani akiwa salama.

“Rais ameviagiza vyombo vya usalama kwamba kwa sababu ni suala la dharura, lazima vihakikishe watoto hawa na wale wote waliotekwa nyara wanarejeshwa nyumbani wakiwa salama,” waziri Idris aliwaambia waandishi wa habari.

Alisema hilo lilijiri kufuatia mkutano wa Baraza la Mawaziri jijini Abuja.

Watu wenye silaha ambao waliwateka nyara wanafunzi 286 na wafanyakazi kutoka shule moja iliyo Kaskazini mwa Nigeria wiki iliyopita wamedai jumla ya Naira bilioni 1 (sawa na Sh83 milioni) ili waachiliwe, msemaji wa familia za mateka na diwani wa eneo hilo aliambia shirika la habari la Reuters.

Waliotekwa nyara ni pamoja na wanafunzi wakubwa na wafanyakazi wa shule hiyo waliotekwa nyara mnamo Machi 7, 2024, katika mji wa Kuriga, katika Jimbo la Kaduna Kaskazini Magharibi mwa Nigeria, katika tukio la kwanza la utekaji nyara nchini humo tangu 2021.