• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 5:22 PM
Madaktari bondeni waruhusiwa kujifua kimasomo, watisha kugoma

Madaktari bondeni waruhusiwa kujifua kimasomo, watisha kugoma

MAGDALENE WANJA NA RICHARD MAOSI

ZAIDI ya madaktari 30 kutoka kaunti tano za kusini mwa Bonde la Ufa wamepokea ruhusa ya kuendeleza masomo yao wakati wa likizo.

Hii ni baada yao kutishia kugoma huku wakiwa wamepatia serikali makataa ya siku 21 kuhusu ombi lao.Wanafamasia pamoja na madaktari wa meno kupitia chama chao cha KMPDU wakiungana na viongozi katika tume zao walithibitisha haya wakisema sio jambo la kufanyiwa mzaha.

Kwa mujibu wa katibu mkuu kutoka ukanda huu Dkt Davji Atella kaunti zote sita zilikuwa zimeshindwa kutekeleza  maagano yao na idara husika kupitia (CBA), hali iliyochochea madaktari kunyimwa fursa ya kujiendeleza kimasomo wakati wa likizo pamoja na kuongezewa cheo.

Dkt Atella alieleza kuwa kaunti tano tayari zemeafikiana kuwaruhusu madaktari kuendeleza taaluma zao pamoja na kuwapandisha cheo isipokua kaunti ya Laikipia ambayo bado haijatoa maoni yake kuhusu mpangilio huu.

“Iwapo Kaunti ya Laikipia haitatupatia majibu kwa muda wa siku 21 tutaitisha mgomo wa madaktari wanaofanya kazi katika eneo hilo hadi waafikiane na matakwa ya madaktari,’’ Dkt Atella alisema.

Hata hivyo taarifa kutoka kwenye idara ya mawasiliano katika kaunti ilieleza kwamba wamekuwa wakitumia takriban milioni 10 kila mwezi kuwagharamia madaktari wanaosoma wakati wa likizo.

Pia waliongezea kwamba kwamba madaktari 20 zaidi wameongezwa ili kujaza pengo la utendaji kazi huku wakisubiri wale walio katika likizo kurejea.

‘’Tumepokea maombi 18 kutoka kwa madaktari walio katika likizo wakiomba kuendelea kulipwa wakiwa likizoni lakini jambo hili limepuziliwa na serikali ya kaunti kutokana na uhaba wa fedha pamoja na uchache wa madaktari,’’ idara ya mawasiliano kaunti ya Laikipia ilieleza huku ikiaminika zaidi ya madaktari 12 tayari wameacha kutoa huduma kabisa wakisingizia kuendeleza masomo yao.

Dkt Atella aliongeza kwamba wataendelea kujadiliana na madaktari kutoka kaunti ya Laikipia hadi watakapofikia mwafaka. Iwapo hawatakubaliana basi madaktari wataanza mgomo rasmi.

Ni hospitali chache zilizowaruhusu madaktari kuendeleza masomo kama Nakuru (13), Kericho(9), Bomet (5) na Narok (3).

Dkt Atella alionya baadhi ya hospitali zinazopanga kuwaruhusu madaktari kupata likizo kwamba hawatalipwa.

“Ni jambo ambalo ni kinyume na sheria kwani bado tunahitaji madaktari wengi tuliowaelimisha bila kuwafuta kiholela,” aliongeza. Eneo la kusini mwa bonde hili la ufa kuna madaktari zaidi ya 600.

You can share this post!

BEATRICE ELACHI: Ghasia ofisini zamsukuma kujificha chooni

Furaha kwa Babu Owino hakimu kuamua hana kesi ya kujibu

adminleo