• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 2:07 PM
WATOTO: Mwanafunzi anayelenga kuwa msanii mtajika nchini

WATOTO: Mwanafunzi anayelenga kuwa msanii mtajika nchini

Na PATRICK KILAVUKA

PURITY Wangari, 10, ni mwanafunzi wa darasa la nne katika Shule ya Msingi ya ACK St Johns, Kangemi, Nairobi. Ni kitindamimba katika familia ya Bw John Mbugua na Bi Rosemary Wangui na  matamanio yake ni kuwa mwanamuziki mtajika siku za usoni.

Hata hivyo, anasema kulifikia lengo hilo, ameazamia kujijenga na kutengeneza barabara yake kwa kuwa kiongozi wa nyimbo na kufuatilia masuala ya muziki kwa makini shuleni na kanisani ambako anajiangaza na kuchochea kipawa chake.

Huongoza nyimbo katika ibada za watoto. Mwaka huu, nyota yake ya jaha iling’ara hadi akawashangaza wanafunzi wengine kwa weledi wake wa kuongoza nyimbo pale ambapo aliiwezesha shule yake kushiriki mashindano ya kitaifa katika kiwango cha 819 H na kutia fora kutokea mashinani hadi ya kitaifa.

Msanii chipukizi stadi Purity Wangari, 10, akionyesha tuzo aliyoshinda wakati wa mashindano ya Kanda ya Nairobi. Picha/ Patrick Kilavuka

Shule ilimaliza ya tano bora kitaifa japo huu ulikuwa mwaka wake wa kwanza kuongoza nyimbo shuleni. Mashindano ya Tamasha za Muziki ya Kitaifa yaliandaliwa Chuo Kikuu cha Dedan Kimathi, Kaunti ya Nyeri.

Alituzwa pia kombe la Kanda ya Nairobi katika mashindano hayo na kuiletea shule ya shime.

Wangari aliongoza kikosi cha wanadensi kuwasilisha wasilisho la Kimarakwet anwani ikiwa Chevukwet linalotumbuizwa na vijana wakati wa sherehe za harusi na kuibuka ya kwanza bora kaunti ya Westlands kabla kunogesha mashindano ya Kanda ya Nairobi na kuibuka washindi akiongoza kikundi chao. Hatimaye shule ikafuzu kitaifa.

Purity Wangari akiwa mwalimu wake Lencer Okoth. Picha/Patrick Kilavuka

Kulingana na mwalimu wake Lencer Okoth, Purity alionesha ukakamavu tokea mwanzo. Wakati alikuwa anataka kujua nani atayeongoza wimbo huo, alikuwa wa kwanza kujitokeza akiwa amejiamini na mwenye imani ya kuchukua jukumu hilo.

“Ujasiri wake ulinionyesha kwamba ataweza! Wimbo huu ulitaka kiongozi mkakamavu sana, mwepesi wa kuukariri na mchangamfu. Na kwa kweli pindi tulipoanza kufanya mazoezi ya wimbo, alikuwa mwepesi sana kuukariri jambo ambalo nilinipa moyo kwamba ataweza,” alieleza Okoth ambaye alimumiminia sifa kwa kukiongoza kikosi chake hadi fainali za kitaifa japo wimbo ulikuwa wa lugha tofuati na take ya mama lakini aliujua kwa muda mfupi sana.

Purity ashika taji katikati ya walimu wake. Picha/Patrick Kilavuka

Fauka ya hayo, alimtaja kama mwanafunzi ambaye ana upevu wa wastani kimasomo huku akijimarisha kila uchao katika masomo na kustawisha talanta yake.

Katika uamuzi wa wakaguzi wa nyimbo, walimsifu kwa kuwa kiongozi dhabiti, sauti mwororo na aliye na ari katika kuongoza wimbo kwa ueledi.

Purity akiongozi kikosi cha wasakataji densi kufanya mazoezi ya wasilisho la Kimarakwet Chevukwe ambalo liliibuka tano bora kitaifa. Picha/Patrick Kilavuka

Wangari aliamusha ari ya kipawa chake akiwa darasa la pili.Amekuwa mshiriki sugu wa ibada za watoto kanisa la ACK St Johns, Kangemi anakoongoza nyimbo pia na kiliwakilisha kanisa katika mashindano ya Dayosisi ya Mlima Kenya na yale vijana ambayo hufanyika kanisa la St James Cathedral, Kiambu.

Msanii huyu chipukizi anaonekana kufuata nyendo za ukoo katika kukiimarisha kipaji chake kwani, ndugu yake Naftali Mbugua aliye mwanamuziki alidokeza kwamba, mwanatalanta huyo hufuatilia nyayo zake unyounyo. Yeye hubaki nyuma baada ya ibada na kufanya mazoezi ya kuimba wakati yeye (Naftali) anafanyisha waimbaji wengine mazoezi kanisani.

Purity akiongoza wenzake. Picha/ Patrick Kilavuka

“Wakati tunafanya mazoezi kwa minajili ya kutumbuiza katika ibada au kwa maandalizi ya nyimbo za mashindano, amekuwa akisalia nyuma kufanya mazoezi nasi hali ambayo imemjenga katika tasnia hii,” anasema nduguye Mbugua ambaye pia mchezaji kinanda hodari kanisani na mwalimu wa nyimbo.

Wangari anasema kipaji chake kimenawiri kwa kumtumainia Maulana, nidhamu na kuyatilia maanani mawaidha na ushauri wa wazazi na walimu ambao wamekuwa wa msaada sana. Anajichochea katika kutunga mistari ya nyimbo japo anasema bado anaelekezwa na nduguye.

Purity apokea maagizo kutoka kwa mwalimu wake Lencer Okoth. Picha/Patrick Kilavuka

Anapenda sana somo la Dini na uraibu wake ni kuruka kamba na kucheza densi.

You can share this post!

PATRICK OTIENDE: Straika wa Kangemi anayepania kufikia...

Kaunti ya Nandi yamtuza Kipchoge ng’ombe, uwanja mpya...

adminleo