Stroberi za ‘chandler’ ni tamu pia kwa upande wa hela
MURAYA Mburu alipoacha kufanya kazi katika Kampuni ya Huduma za Maji na Usafi ya Nakuru (NAWASSCO) mwaka 2012 alijitosa katika kilimo shambani mwake Nyakiambi mjini Elburgon, Kaunti ya Nakuru.
Tulipomtembelea majuzi tulimpata katika pilkapilka za kuvuna na kupakia mavuno ya matunda ya stroberi kwa ajili ya kuyauza.
“Baada ya kuzalisha mahindi kwa miaka mitano nilififia kwani kilimo hicho hakikuwa kikienda vizuri.
Baada ya kuuza mahindi makavu niliyokuwa nayo nilinunua kondoo dume 12 kwa kati ya Sh3,000 na Sh 5,000 kila mmoja kulingana na saizi.
Nikawalea kwa mwaka mmoja kabla kuwauza Sh9,000 kila moja,” alitanguliza Muraya kuhusu safari yake ndefu ya kilimo na ufugaji.
Akapata ugumu kulea kondoo zaidi kutokana na uhaba wa malisho.

Ni wakati akikuna kichwa alipokumbuka makala katika chapisho la awali la Akili Mali, jinsi wakulima walikuwa wakistawi kwa kuuza bidhaa zao mtandaoni.
Pitapita zake zikampeleka kwa kilimo cha stroberi. Akabaini ni rahisi kuanzisha, hakikuwa na kazi nyingi, na matunda yalichukua miezi michache kukomaa, tofauti na mahindi ambayo huchukua karibu mwaka mzima.
Pia aligundua mauzo ya stroberi yalikuwa mazuri hata katika soko la mashinani.
Muraya akafuatilia wakulima wa matunda hayo na kutembelea baadhi waliochapisha bidhaa zao mtandaoni. Ni kutoka kwa mmoja alijifunza kuhusu aina za stroberi zilizofaa maeneo mbalimbali.
“Mnamo 2019 nilitembelea mkulima mjini Nyahururu, Kaunti ya Laikipia, nikanunua miche 800 kabla baadaye kuongeza 800 zaidi, kila moja ikiwa Sh30, kutoka kwa mtaji wa Sh120,000 niliokuwa nao,” asema na kuongeza kuwa alihakikishiwa miche hiyo ilikuwa bora na ingenawiri eneo lake.
Alitumia pesa zilizobaki kununua matangi ya maji, mabomba, kutayarish shamba, na nyavu ili kuepusha ndege wasifikie matunda shambani.
Baada ya kukuza miche kwa mwezi mmoja aliipandikiza katika shamba lake la nusu robo.
“Kwa kuwa sikuwa na mbolea ya kinyesi cha kondoo, ambayo ilikuwa bora kuchanganya na udongo wakati wa kupanda, niliweka ile ya kutokana na kinyesi cha ng’ombe baada ya wiki tatu,” aeleza.
Aliendelea kumwaga maji kwa miche hiyo kila asubuhi na jioni hasa wakati hakuna mvua, lakini baada ya miezi miwili alikuwa akitia maji mara mbili pekee kila wiki.
Muraya anasema spishi ya chandler ambayo ndiyo anakuza katika shamba lake hustahimili hali ya anga ya eneo la Elburgon na Molo, ambayo mara nyingi ni baridi na mvua.
Hata hivyo, atahadharisha kuwa mvua nyingi ni tatizo kwani matunda hupenda kiangazi wakati wa kukomaa.
“Ningeomba serikali ya kaunti iimarishe mafunzo kwa wakulima kuhusu upanzi na soko la stroberi ili wapate mapato mazuri. Matunda haya ni matamu na utamu huo umefanya wateja kuongezeka, ikiwemo wakulima wanaonunua miche kwa upanzi,” aeleza.
Ni ombi ambalo Waziri wa Kilimo wa Kaunti ya Nakuru Leonard Bor, amelisikia kwani anasema maafisa wa kilimo nyanjani wako tayari kufika kokote katika kaunti ili kuhamasisha wakulima kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo mifumo faafu ya kilimo, maradhi ya mimea, kudhibiti wadudu waharibifu na kadhalika.
“Kama serikali ya kaunti tutaimarisha mipango ya kuhamasisha na kuwafikia wakulima wengi hususan siku za kilimo au kuwatembelea mashambani mwao ili kuendelea kufanikisha kilimo,” alisema Bor na kuongeza kuwa wakulima pia huarifiwa wakati wa siku za kilimo kupitia ofisi za chifu katika maeneo yao.
Muraya anahoji kwamba soko la matunda limeongezeka pakubwa katika maeneo ya Molo, Elburgon na Kuresoi tangu janga la corona kutokana na himizo la wataalamu wa afya kwamba matunda yana virutubishi ambavyo huimarisha kingamwili, na hivyo kusaidia kupambana na homa hiyo.
Mavuno yake ya kwanza yalikuwa ya kuridhisha, lakini mwanzoni alipata changamoto kuyauza katika soko la mashinani kwani stroberi bado zilikuwa hazijachangamkiwa sana.
Akaanza kupakia katika vikontena vidogo vya plastiki vya kuweka vyakula kavu [punnets kwa Kimombo] kwa wateja wa mijini na baadaye maduka makubwa ya jumla.
Hata hivyo, aliendelea kuuza matunda yake reja reja kwa kutembea kutoka sehemu moja hadi nyingine kutokana kwamba baadhi ya wateja na maduka hayakuwa na friji za kuhifadhi matunda hayo katika vikontena.
Sasa anafurahia matunda ya bidii yake kwani soko lake limeendelea kunawiri katika mji wa Elburgon na viunga vyake.
Mkulima huyu hana majuto tangu alipozamia kilimo cha stroberi miaka saba iliyopita kwani amefanikiwa kumudu karo ya shule ya watoto wake na kukidhi mahitaji mengine ya kimsingi nyumbani.
“Msimu mzuri ninavuna mara mbili kwa wiki, kati ya paneti 40 na 60 na kuuza kila kifurushi Sh150,” alisema Muraya na kuongeza kuwa mpango wake ni kufuga kondoo ambao watamsaidia kupata mbolea asilia, ambayo ndiyo yeye hutumia shambani.
Aidha, maono yake katika siku zijazo ni kupanua shamba hadi ekari tano akitumai soko la stroberi litaendelea kunawiri eneo hilo na kote nchini.