Habari za Kitaifa

NTSA: Vifo vingi barabarani vyasababishwa na magari ya kibinafsi na malori

Na WINNIE ONYANDO August 2nd, 2024 1 min read

RIPOTI mpya ya Mamlaka ya Kitaifa ya Usalama Barabarani (NTSA) imetupilia mbali kasumba kuwa nyingi za ajali barabarani husababishwa na magari ya abiria.

Kwa mujibu wa ripoti ya hivi punde ya NTSA, idadi kubwa ya vifo barabarani husababishwa na magari ya kibinafsi na malori.

Hii ni tofauti sana na ripoti za hapo awali ambazo zimekuwa zikionyesha kuwa maafa mengi barabarani husababishwa na magari ya abiria.

Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa licha ya ukweli kwamba pikipiki zilisababisha vifo vingi barabarani mwaka uliopita hadi mwezi Juni 2023 (vifo 1,157), magari ya abiria yalifuatia kwa vifo 1,086 ilhali magari ya kibinafsi yalisababisha vifo 1,078.

Magari ya serikali yalisababisha vifo 57 huku ambulensi zikisababisha vifo viwili kisha mkokoteni kifo kimoja.