TAHARIRI: Msamaha wa Ruto kwa Gen Z uambatane na vitendo, haki
OMBI la msamaha ambalo Rais William Ruto alielekeza Jumatano kwa Gen Z linastahili kuandamana na vitendo la sivyo litachukuliwa kama matamshi ya kawaida ya kisiasa ambayo yamewahi kutolewa awali kusaka umaarufu.
Pia, wito wake wa umoja wa nchi uliolenga mirengo mbalimbali ya kisiasa unastahili kudhihirika katika uongozi wake.
Jana, katika ibada ya kila mwaka ambayo hupangwa na kuandaliwa na Bunge, Rais alionekana kunyenyekea na kuwaomba Gen Z msamaha.
Alisema iwapo kuna mahala popote ambao utawala wake umewakwaza, basi anawaomba msamaha na akawasihi waungane kwa ajili ya umoja wa taifa.
Akihutubu na kuzungumzia masuala ya Gen Z na umoja wa nchi, Rais alionekana kunyenyekea sana na kuwa muungwana kinyume na hapo awali ambapo amekuwa akionekana kutoshughulishwa na maasi ya vijana.
Hata hivyo, kuomba msamaha kwa Gen Z kutakuwa wa maana iwapo msamaha huo utaandamana na vitendo vya kutii wito na matamanio ya vijana nchini.
Tangu maandamano ya Gen Z mwaka jana, makovu ya maafa na majeraha ambayo yalitokea bado yapo.
Vijana hawajapona kutokana na dhuluma ambazo walipitia mikononi mwa vikosi vya usalama.
Kuonyesha kuwa msamaha huo ni wa kweli, Rais anastahili kuamuru fidia ilipwe kwa wale ambao walipoteza mali yao mikononi mwa maafisa wa usalama na wale ambao walijeruhiwa.
Pili, kuna familia ambazo vijana wao walitekwa nyara wakati wa maandamano ya Gen Z na hata kwenye wimbi la utekaji nyara ambalo limekuwa likishuhudiwa nchini.
Awali, Rais aliamuru kuwa wote ambao walikuwa wametekwa nyara wangeachiliwa lakini ahadi hii haijatimia.
Kuna vijana wawili waliotekwa nyara Mlolongo na hadi leo hawajawahi kupatikana miongoni mwa wengine ambao familia zao bado zinawasaka.
Iwapo wote waliotekwa nyara wataachiliwa, basi ndipo itaaminika kuwa ombi la msamaha la rais lilifanyika kwa roho safi.
Aidha, kuna polisi ambao walitumia mamlaka yao vibaya na kuwapiga risasi vijana kiholela.
Hawa walienda kinyume na maadili au utendakazi wao na wanastahili wachukuliwe hatua kali za kisheria kwa kufungwa.
Msamaha wa Rais pia unastahili kuonekana kwenye utendakazi wa serikali hasa kuhusiana na kusuluhisha changamoto zinazowasibu vijana.
Aagize maafisa wakuu serikalini wachunge ndimi zao na wakome kudhalilisha vijana, uteuzi wake ushirikishe vijana kwenye nyadhifa mbalimbali, akomeshe ufisadi.