Habari

Wanasiasa sasa wang’ang’ania Gen Z wakiunda nafasi za kujikimu

Na JUSTUS OCHIENG June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MNG’ANG’ANIO wa kura za vijana wa Gen Z kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 umeshika kasi huku serikali ikianzisha mpango mwingine wa kuwawezesha vijana ili kuimarisha maisha yao.

Serikali inaanzisha mpango huo kwa jina, “National Youth Opportunitu Towards Advancement (NYOTA), wakati ambapo vyama vya kisiasa na wagombeaji urais wakiongeza juhudi za kuvutia kura za vijana kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao.

Akihutubu alipoongoza sherehe za kitaifa za Madaraka Dei, mjini Homa Bay, Jumapili, Rais William Ruto alieleza kuwa mpango wa NYOTA inalenga kuwawezesha jumla ya vijana 800,000 wenye umri wa kati ya miaka 18 na 29 na hadi miaka 35 kwa wale wanaoishi na ulemavu.

“Serikali kwa ushirikiano na Benki ya Dunia inaanza mpango wa NYOTA utakaogharimu Sh20 bilioni kusaidia vijana kwa kutambua mchango katika ukuaji wa uchumi wa taifa hili,” akasema.

“Uwezeshaji huo utafikiwa kupitia mafunzo ya ziada yatakayowawezesha vijana kupata ajira au nafasi ya kujiajiri baada ya kukamilisha masomo. Aidha, chini ya mpango huu vijana wenye ujuzi wa kiufundi watatambuliwa na kupewa vyeti vya kuhitimu, watapewa mafunzo ya ujasiriamali na umuhimu wa kuweka akiba,” Dkt Ruto akasema katika uwanja wa michezo wa Raila Odinga.

Kiongozi wa taifa alieleza kuwa mpango huo wa NYOTA unalenga kufaidi vijana 70 katika kila wadi kote nchini kwa kupata ruzuku, mafunzo ya kibiashara na masoko bora kwa bidhaa wanazotengeneza.

“Kuanzia Agosti mwaka huu tutatoa Sh5 bilioni, kama awamu ya kwanza ya ufadhili huo, kufaidia jumla ya vijana 100,000, kila mmoja akipokea Sh50,000 za kuanzishia biashara,” Dkt Ruto akaeleza.

Kiongozi wa taifa aliendelea kuwavutia vijana kwa kutangaza kuwa kuanzia wiki hii, serikali itaanza mpango kutoa ajira kwa vijana, maarufu kama “Climate Worx”, zamani ikiitwa, “Kazi Mitaani”.

“Chini ya mpango huo tutawasajili jumla ya vijana 110, 000 katika kaunti 46 kwa kazi za ujenzi, utunzaji wa usafi wa mazingira na upanzi wa miti. Tutazipa kipaumbele vitongoji duni katika miji mikubwa na vijiji katika kaunti za mbali,” Dkt Ruto akaeleza.

Mpango huo wa Climate Worx ulianzishwa katika kaunti ya Nairobi mwaka jana ambapo vijana 3, 500 walisajiliwa na wamefaidi pakubwa tangu wakati huo.

Huku uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia, vijana wa Gen Z wameondokea kuwa kundi kubwa lenye idadi kubwa ya kura.

Mwaka jana, tabaka hili la Wakenya waliozaliwa kati ya 1997 na 2010, walithibitisha kuwa wanajali maswali ya uongozi wa taifa hili walipoungana kupinga Mswada wa Fedha wa 2024.

Baada ya maandamano waliofanya katika takriban kaunti 36 nchini Gen Z walifaulu kuiwekea serikali presha hadi Rais Ruto akatupilia mbali vifungu vyote vya mswada huo.